Dk Nchimbi atua Mwanza kwa kampeni

MWANZA; MGOMBEA mwenza wa Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi, amewasili jijini Mwanza kwa ajili ya kampeni za chama hicho na kupokelewa kwa shangwe kubwa na viongozi pamoja na wanachama wa CCM mkoani humo.
Mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Mwanza, Dk. Nchimbi alitia saini kitabu cha wageni na kupata maelezo mafupi kutoka kwa viongozi wa chama mkoani humo, kabla ya kutoa shukrani zake kwa mapokezi makubwa aliyoyapata yeye na timu yake.
Alisema yupo tayari kuendelea na kampeni na kutangaza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2025–2030, akisisitiza chama kimejipanga kuhakikisha maendeleo ya Watanzania yanapewa kipaumbele.
Baadaye, Dk. Nchimbi anatarajiwa kufanya mikutano midogo na wananchi wa wilaya za Kwimba na Ilemela, kabla ya kuhutubia mkutano wa hadhara utakaofanyika jioni katika viwanja vya Furahisha jijini humo.