Waangalizi wa EAC waingia Tanzania

JUMUIYA ya Afrika Mashariki (EAC) imezindua Timu ya Uangalizi wa Uchaguzi yenye wataalamu 67 kutoka nchi zote wanachama, kwa ajili ya kufuatilia na kusimamia Uchaguzi Mkuu wa Tanzania unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29, 2025.
Timu hiyo itaongozwa na Dk. Speciosa Kazibwe, aliyewahi kuwa Makamu wa Rais wa Uganda kati ya mwaka 1994 hadi 2003, ambaye pia anajulikana kama mwanamke wa kwanza barani Afrika kushika wadhifa huo katika taifa huru. SOMA: Watu milioni 5 hufariki tezi dume kwa mwaka EAC
Uzinduzi wa Timu hiyo imefanyika jijini Dar es Salaam kufuatia mwaliko wa Serikali ya Tanzania, sambamba na maagizo ya Baraza la Mawaziri la EAC yanayoitaka Sekretarieti ya Jumuiya kushiriki katika uangalizi wa chaguzi za nchi wanachama.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dk. Kazibwe amesema jukumu kuu la Timu ni kutathmini mwenendo wa uchaguzi kwa mujibu wa sheria za nchi, lizi kanuni za EAC za uangalizi wa uchaguzi na viwango vya kimataifa vya uchaguzi huru na wa haki. “EAC inaamini kuwa uchaguzi huru na wa haki ni nguzo kuu ya demokrasia na ushirikiano wa kikanda. Jumuiya imejengwa juu ya misingi ya utawala bora, utawala wa sheria na kuheshimu haki za binadamu,” amesema Dk. Kazibwe.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa EAC, Veronica Nduva, amesema Tume hiyo itatoa taarifa ya awali muda mfupi baada ya uchaguzi, ikifuatiwa na ripoti kamili itakayobainisha matokeo ya uangalizi na mapendekezo ya kuboresha chaguzi zijazo.
Naye Naibu Kiongozi wa Timu hiyo, Maina Karobia, ambaye pia ni Mjumbe wa Bunge la EAC (EALA), amesema kazi ya waangalizi si kuingilia uchaguzi bali kufuatilia kwa uwazi na uadilifu. “Timu itahakikisha mchakato wa uchaguzi unakuwa wa amani, uwazi na kuaminika, na tutashirikiana kikamilifu na wadau wote,” amesema.
Kuzinduliwa kwa Tume hiyo kunatekeleza masharti ya Kifungu cha 6(d) cha Mkataba wa EAC, kinachozitaka nchi wanachama kudumisha misingi ya utawala bora ikiwemo demokrasia, uwajibikaji, usawa wa kijinsia, uwazi na kuheshimu haki za binadamu kwa mujibu wa Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu.



