KATIKA kipindi cha mwaka wa fedha 2024/25 Halmashauri ya Wilaya ya Longido mkoani Arusha imetenga Sh milioni 229 kwa ajili mikopo kwa vijana,wanawake na watu wenye walemavu.
Akizungumza na HabariLEO, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Longido, Nassoro Senzigwa amesema kuwa kiwango hicho cha fedha ni asilimia 10 ya makusanyo ya mapato ya ndani yaliyokusanywa kutoka katika vyanzi mbalimbali vilivyopo katika halmashauri hiyo.
Senzigwa amesema kuwa tayari vikundi 15 vilivyokidhi vigezo vimeshakopeshwa ikiwa ni pamoja na kukidhi vigezo viliwekwa kwa mujibu wa taratibu mpya za serikali.
Amesema katika vikundi hivyo 15 vilivyokopeshwa ni pamoja na vikundi sita vya wanawake,vikundi saba vya vijana na vikundi viwili vya watu wenye walemavu.
Mkurugenzi huyo amesema kuwa jumla ya Sh milioni 181 zimeshakopeshwa kwa mchanganuo wa shilingi milioni 80.5 vikundi vya wanawake Sh milioni 80.5 vikundi vya vijana na Sh milioni 20 kwa vikundi vya watu walemavu.
‘’Fedha zilizotolewa zimetokana na asilimia 10 ya mapato ya ndani ya Halmashauri ya Longido na marejesho ya mikopo ya nyuma,” amesema Senzigwa.
Naye Ofisa Maendeleo ya Jamii wa Halmashauri ya Longido, Grace Elia amesema kuwa vikundi vyote vilivyokopeshwa fedha hizo vimehimizwa kuzingaatia sheria na kanuni za mikopo na kusema kuwa wataokiuka taratibu za kisheria zitahusika.
Amesema mkakati wa Halmashauri ni kuendelea kuimarisha hali ya uchumi kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kwa kuwajengea uwezo kupitia mafunzo mbalimbali ya ujasilimali, kutengeneza mazingira rafiki ya uendeshaji wa biashara na kufungua fursa mbalimbali za kiuchumi kwa vikundi vyote wilayani humo.
Mbunge wa Jimbo la Longido,Dk Steven Kiruswa alivitaka vikundi hivyo kuzingatia mikopo waliyokopa ikiwa ni pamoja na kurejesha kwa wakati ili vikundi vingine viwezee kukopesheka kwa kuzingatia taratibu zilizopo.
Kiruswa ambaye pia ni Naibu Waziri wa Madini aliviasa vikundi kuzingatia taratibu za kukopa zilizowekwa na serikali baada ya kufanyiwa maboresho kwani masharti haayo yasipofuatwa yanaweza kuwaweka katika mazingira magumu.
“Kila anayekopa anapaswa kufuata masharti ya kukopa ikiwa ni pamoja na kurejesha mkopa kwa wakati” amesema Kiruswa.