Serikali yazitaka DSE, TCB kuwawezesha wananchi kuwekeza
DAR ES SALAAM: Serikali imeliagiza Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) na Benki ya TCB kuhakikisha kwamba Watanzania wanapata elimu ya kutosha kuhusu umuhimu wa kuwekeza katika soko la mitaji kwani ni njia muhimu ya kuongeza ushiriki wa wananchi katika uwekezaji wa hisa na hatimaye kuchochea ukuaji wa uchumi na kusaidia sekta binafsi kupata mtaji wa muda mrefu kwa njia endelevu.
Agizo hilo lilitolewa na Msajili wa Hazina, Nehemia Mchechu wakati akizindua huduma ya uwekezaji wa hisa kupitia ‘Popote Mobile App’ na kuiagiza TCB kuhakikisha huduma hiyo mpya inakuwa rahisi, salama na inapatikana kwa wananchi wote bila vikwazo vya kiufundi.
Alitumia fursa hiyo kuiagiza DSE na benki zishirikiane kupunguza gharama za uwekezaji na kuongeza ufanisi wa miamala ya hisa kwa kutumia mifumo ya kidijitali kwani Serikali inalenga kuimarisha ushiriki wa wananchi katika masoko ya mitaji na kuchochea maendeleo ya uchumi wa soko huria nchini.

Naye ofisa mtendaji mkuu wa TCB, Adam Mihayo, ameeleza kuwa uzinduzi wa Popote Mobile App ni hatua muhimu katika kuimarisha ujumuishaji wa kifedha na kuleta mageuzi katika soko la mitaji nchini na kuwa kuunganisha mifumo ya benki na DSE ni kunapanua wigo wa uwekezaji kwa kurahisisha upatikanaji wa hisa kwa wawekezaji wa rika zote huku ikiongeza ukwasi katika soko la hisa na kuvutia wawekezaji wapya.
Akizungumza katika tukio hilo, Mtendaji Mkuu wa DSE, Peter Nalitolela alisema kuwa teknolojia hii inarahisisha ununuzi na uuzaji wa hisa moja kwa moja kupitia simu za mkononi, bila kulazimika kutembelea madalali wa hisa au ofisi za soko jambo linalopanua wigo wa ushiriki wa wananchi katika soko la mitaji na kusaidia kampuni zinazoorodheshwa kupata mtaji.
ALSO READ: KARNE YA HUDUMA: TCB yajipambanua kidijitali
hata hivyo, Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMA), Nicodemus Mkama aliipongeza TCB kwa kuja na ubunifu huyo akieleza kuwa hiyo ni hatua muhimu katika kuhakikisha Watanzania wanapata urahisi wa kuwekeza kupitia teknolojia ya kidijitali,kwani teknolojia hii inawawezesha kufanya miamala ya hisa kwa njia salama na rahisi, bila vikwazo vya kifedha au kijiografia.
Uzinduzi wa huduma hii unakuja katika wakati ambapo soko la mitaji la Tanzania linahitaji mageuzi ya kidijitali ili kuongeza ushiriki wa wananchi.
Programu hiyo inatajwa kuwa ni suluhisho la kisasa ambalo linaruhusu Watanzania kufanya miamala ya hisa kupitia simu zao za mkononi na kuchochea ukuaji wa uchumi na kupanua fursa za uwekezaji katika masoko ya mitaji.



