KAMISHNA Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Yusuph Mwenda ametoa tuzo ya heshima kwa kampuni ya uzalishaji wa vinywaji changamshi ya Mati Super Brands limited ambao ni walipa kodi wakubwa. Kwa miezi mitano kampuni hiyo imelipa kodi ya Sh bilioni 5.
Mwenda amesema hayo alipotembelea kiwanda cha Mati Super Brands Limited mjini Babati mkoani Manyara na kujionea shughuli mbalimbali za uzalishaji wa vinywaji vyenye ubora wa kitaifa na kimataifa.
Mwenda amesema kuwa kampuni hiyo ni miongoni mwa walipa kodi wakubwa nchini hivyo TRA itaendelea kutoa ushirikiano ili kuhakikisha kampuni hiyo hiyo yenye mchango mkubwa kwa taifa inazidi kukua na kufikia malengo yake.
“Sisi kama TRA tuko tayari kutoa ushirikiano wa kutosha kwa kampuni ya Mati Super Brands Limited na kuhakikisha tunatatua changamoto zinazowakabili ili iendelee kufanya vizuri zaidi,” ameeleza Kamishna Mkuu.
Mkurugenzi wa Kampuni ya Mati Super Brands Limited David Mulokozi ameipongeza TRA Kwa kutoa ushirikiano mkubwa kuiwezesha kampuni hiyo kukua kwa kasi na kuongeza kasi ya usambazaji wa bidhaa zake ndani nan je ya nchi.
Mulokozi amesema kuwa kwasasa wameanza kupeleka bidhaa zao katika masoko ya nchi za Congo, Zambia na Malawi.Aidha amesema kuwa kampuni hiyo itaendelea kuzalisha bidhaa bora zenye viwango vya kitaifa na kimataifa.