Umoja wa kitaifa utalinda amani ya nchi

TAASISI za kidini na kielimu kwa kushirikiana na Kituo cha Utamaduni cha Ubalozi wa Iran zimeandaa mdahalo maalumu wenye lengo la kudumisha amani, mshikamano, utulivu na haki kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29 mwaka huu. Mdahalo huo umefanyika leo jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa mdahalo huo, Kiongozi Mkuu wa Kanisa la Evangelical Fellowship Church Tanzania, Askofu Charles Asher, amewataka wananchi kutumia haki yao ya kikatiba kwa amani kuchagua viongozi wanaowataka. “Tanzania imeendelea kuwa mfano wa utulivu na umoja tangu ilipopata uhuru mwaka 1961”, alisema Askofu Asher.

Aidha, amewataka Watanzania kutumia mitandao ya kijamii kwa busara, na kuepuka kuvitumia kama majukwaa ya uchochezi au kuvunja amani, akisisitiza umuhimu wa kuilinda heshima ya taifa hasa wakati wa uchaguzi. SOMA: Samia: Vijana lindeni amani

Kwa upande wake, Sheikh Mulaba Saleh Lulat, Mwenyekiti wa Taasisi ya Safina Salamar, amesisitiza umuhimu wa kulinda tunu ya amani ambayo imejengwa kwa misingi imara na mizizi iliyowekwa na viongozi wa dini pamoja na wazee wa taifa. “Ni wajibu wa kila mtanzania kutambua mambo mema na kuachana na yale yanayoweza kuvuruga umoja wa taifa”,alisema.

Naye Mkurugenzi wa Kituo cha Utamaduni cha Ubalozi wa Iran, Dk. Mohsen Maarefy, amesema majadiliano kama hayo ni muhimu katika kuimarisha mshikamano wa kitaifa na kudumisha amani. Mdahalo huo umetajwa kuwa sehemu ya jitihada endelevu za wadau wa dini na elimu katika kujenga jamii yenye hekima, umoja na maadili kuelekea uchaguzi wa amani.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button