Watoto 4,000 wanahitaji matibabu ya moyo

DAR-ES-SALAAM : TAKRIBAN watoto 10,000 huzaliwa na matatizo ya moyo nchini kila mwaka ambapo kati yao, 4,000 huhitaji upasuaji wa haraka. Hii ni sawa na mtoto mmoja kati ya kila watoto 100, amesema Mkurugenzi wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Dk. Peter Kisenge.
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam wakati wa maadhimisho ya Siku ya Moyo Duniani, alisema JKCI inatoa huduma za bure za uchunguzi wa moyo kwa siku tatu katika tawi la Dar Group, na hadi sasa zaidi ya watu 220 wamejitokeza kupata huduma hizo.
Dk. Kisenge alisema magonjwa ya moyo yanaongezeka kwa kasi duniani na zaidi ya watu milioni 20 wamepoteza maisha. Alisema maadhimisho hayo yamewekwa ili kutoa elimu kwa wananchi kuhusu namna ya kujikinga na magonjwa hayo. “Sababu nyingi za magonjwa ya moyo zinazuilika. Miongoni mwao ni kutofanya mazoezi, uvutaji sigara, unywaji pombe uliokithiri na ulaji wa vyakula visivyozingatia lishe bora,” alisema.
Aliongeza kuwa ulaji wa nyama nyekundu na vyakula vyenye mafuta kwa wingi bila mazoezi unasababisha ongezeko la uzito na hatimaye magonjwa ya moyo. Aidha, magonjwa nyemelezi kama kisukari na shinikizo la damu huchangia kwa kiasi kikubwa.
Akizungumzia watoto, alisema baadhi huzaliwa na matatizo ya moyo endapo mama mjamzito hutumia pombe au sigara kupita kiasi, kukosa chanjo ya magonjwa nyemelezi, au kutumia dawa bila maelekezo ya daktari. Aliwashauri wajawazito kula vyakula vyenye folic acid na kuepuka dawa zisizoelekezwa na wataalamu wa afya.
Aidha, alisema wananchi wanashauriwa kufanya mazoezi, kupima afya mara kwa mara na kujua kiwango cha mafuta, sukari na shinikizo la damu ili kujikinga na maradhi hayo. JKCI pia imeanzisha programu ya Dk. Samia Outreach Programme ambapo wamezunguka mikoa 23 na kuwafikia zaidi ya watu 23,000 kwa kutoa elimu na huduma za uchunguzi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa JKCI – Dar Group, Dk. Tulizo Shemu alisema zaidi ya asilimia 60 ya magonjwa yasiyoambukiza nchini yanaongozwa na matatizo ya moyo. Alibainisha kuwa mara nyingi wagonjwa hawana dalili na hujikuta wakipata matatizo ghafla. SOMA: Bima ya Afya kwa Wote kutibu figo, moyo
“Shida ya moyo ikishindikana, gharama zake ni kubwa. Kuzibua mshipa mmoja ni Sh milioni sita, kifaa cha umeme wa moyo ni Sh milioni 10 na kifaa cha moyo ukikwama kabisa ni Sh milioni 30. Hii yote inaweza kuzuilika kwa kuchunguza afya angalau mara mbili kwa mwaka,” alisema. Daktari bingwa wa moyo kwa watoto, Dk. Eva Kuganda alisema wamewapima watoto zaidi ya 25 na watano kati yao wamebainika na matatizo ya moyo ya kuzaliwa bila kuwa na dalili.