Wazee watunzwe kulinda utu wa kila Mtanzania

KILA mwaka Oktoba Mosi, dunia huadhimisha Siku ya Wazee Duniani ikilenga kuchota hekima, kutambua umuhimu wao na kuendelea kulinda utu na heshima yao.

Aidha, maadhimisho haya pia yanabeba taswira ya wazi kwa kundi hili, yakionesha jinsi wazee walivyotumia nguvu zao kulijenga taifa na ulazima wa kuwathamini leo wakati nguvu zikiwa zinawaishia.

Umuhimu wa kundi hili mwaka huu unajidhihirisha pia kupitia Kaulimbiu isemayo, ‘Wazee Wanaendesha Hatua za Kijamii na Kimaisha: Matamanio Yetu, Ustawi Wetu na Haki Zetu’.

Kaulimbiu hii inatufundisha kuwa wazee si wapokeaji wa huduma pekee, bali wana mchango mkubwa katika shughuli za maendeleo kutokana na kile walicholifanyia taifa na hekima walio nayo inayotosha kutoa mwelekeo wa taifa siku zijazo.

Katika ujumbe wake kwa siku hiyo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), António Guterres ameeleza idadi ya watu wenye umri wa zaidi ya miaka 60 imeongezeka mara mbili katika miongo mitatu iliyopita na sasa imefikia watu bilioni 1.2.

Takwimu za dunia zinaeleza ikifika mwaka 2050, wazee wengine milioni 900 wataongezeka na kuifanya idadi hiyo kuwa kubwa duniani kote.

Kwa kauli hii ya Guterres na takwimu hizi, ina maana wazee ni kundi muhimu kwa mustakabali wa taifa lolote.

Hivyo, wanapaswa kutizamwa kwa jicho la kimaendeleo, kulindwa afya zao na kutumiziwa mahitaji yao ya msingi.

Tunaamini hapa nchini watendaji wataendelea kufanyia kazi sera na miongozo inayogusa kundi hili, ikiwepo kuwapa wazee kipaumbele katika maeneo muhimu kama hospitalini, kwenye taasisi za fedha na vyombo vya usafiri.

Tunashauri ili kuwaenzi, daima wazee wasiachwe nyuma katika shughuli za kimaendeleo, kwani bado busara na hekima zao zinahitajika katika jamii. Waswahili wana msemo usemao, “Ukubwa Dawa”.

Msemo huu unalilenga kundi hili na kwa hakika jamii yenye maendeleo inao wazee wenye hekima na busara wanaotumika sawasawa katika ngazi za familia, jamii na taifa.

Tunasisitiza jamii iwatunze wazee kwa mustakabali bora wa taifa la sasa na lijalo.

Tunazikumbusha familia kuwatunza wazazi waliofikia uzee kwa kuwatendea mema, kuwafurahia, kuhakikisha usalama wao kiroho na kimwili, chakula bora, malazi na huduma za afya, huku wakikumbuka kuwa nao ni wazee
watarajiwa.

Aidha, serikali, familia na taasisi binafsi zinapaswa kushirikiana kuhakikisha wazee wanapata huduma bora za
afya, msaada wa kisaikolojia na heshima inayostahili popote wanapokuwa.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button