Makongoro aibuka mshindi safari ya Kombe la Dunia

DAR ES SALAAM:MAKONGORO Nyerere, mtoto wa Baba wa Taifa Julius Nyerere, ameingia katika orodha ya washindi watatu wa droo ya kampeni ya Kombe la Dunia ya benki ya CRDB hatua ambayo imezua mvuto wa kipekee kutokana na historia ya familia yake nchini.
Makongoro alitangazwa mshindi wa safari ya kushuhudia michuano ya Kombe la Dunia 2026 itakayofanyika Canada, Marekani na Mexico, na baada ya kupigiwa simu kuthibitishiwa ushindi wake alijibu kwa kifupi: “Asante sana.”
Ushindi wake umeonekana kubeba taswira ya kipekee ya urithi wa familia ya Nyerere, ambapo jina la Baba wa Taifa linaendelea kuhusishwa na matukio makubwa ya kitaifa na kimataifa hata katika nyanja tofauti kama michezo na burudani.
Wengine waliobahatika katika droo hiyo ni mfanyabiashara maarufu Arun Lodhia pamoja na Abdulraouf Suleiman, ambao nao wataungana katika safari hiyo ya kihistoria ya kushuhudia Kombe la Dunia.
Katika upande wa zawadi za vifaa vya elektroniki, washindi wa televisheni ni Arina Kaswala, Lusekelo Michael na Easter Kabakama.
Akizungumza wakati wa droo hiyo iliyofanyika Dar es Salaam, Karington Chahe amesema kampeni hiyo imeendelea kuwapa nafasi wateja wa benki hiyo kushiriki ndoto ya kushuhudia Kombe la Dunia moja kwa moja.

Amesema jumla ya washindi 20 wanatarajiwa kunufaika na kampeni hiyo, ambapo 10 watasafiri kwenda Marekani na Canada, huku wengine wakipata zawadi mbalimbali zikiwemo televisheni za inchi 85 na ving’amuzi.
“Fursa ya Kombe la Dunia ipo kwa Watanzania kupitia matumizi ya TemboCard. Kampeni hii inaendelea na mwezi ujao tutapata washindi wengine watakaokwenda kushuhudia mashindano hayo,” amesema.
Kombe la Dunia 2026 linatarajiwa kufanyika katika nchi tatu za Marekani, Canada na Mexico, likiwa moja ya matukio makubwa zaidi ya michezo duniani.
CRDB Bank imesema kampeni hiyo ni sehemu ya kurudisha fadhila kwa wateja wake pamoja na kuongeza hamasa ya matumizi ya huduma zake za kidijitali.



