Gharama za maji zizingatie uchumi wa wananchi

Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) wilayani Iringa, wametakiwa kupanga bei za maji zinazoendana na hali ya uchumi wa wananchi, ili kila mtanzania aweze kusogezewa huduma ya maji safi na salama nyumbani kwake.

Rai hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi RUWASA, Mhandisi Ruth Koya akiwa katika ziara yake ya kikazi mkoani Iringa.

“Kumbukeni maji hayana mbadala na lengo la serikali ni kuhakikisha wananchi wote wanapata huduma ya maji katika umbali usiozidi mita 400, hivyo uwepo wa miradi ya maji karibu na wananchi lazima uendane na gharama za kupata maji kwa kuzingatia hali ya kiuchumi ya wananchi- msipandishe bei hovyo kama soda,” alisema Mhandisi Koya.

Mbali na bei, Mhandisi Koya aliiagiza RUWASA) wilayani humo kuhakikisha inasogeza huduma ya maji katika maeneo ya wafugaji kwa ajili yao na mifugo yao.

Amesema kukosekana kwa huduma hiyo katika maeneo ya wafugaji kumechochea baadhi yao kuharibu miundombinu ya maji inayopita jirani nao ili wajipatie huduma hiyo na kwa ajili mifugo yao.

“RUWASA watendeeni haki wafugaji,  wasogezeeni huduma ya maji; wafugaji siyo masikini mkiwasogezea huduma hii watalipia na hawataharibu miundombinu yake,” alisema.

Awali Diwani wa Viti Maalumu  Tarafa ya Isimani (Walipo wafugaji wengi) Yusta Mkinyaga alithibitisha ni kweli baadhi ya wafugaji wamekuwa wakikata mabomba ya maji ili wapate sehemu za kunywesha jambo linalosababisha hasara kwa RUWASA.

“Yapo maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya mifugo kunywa maji lakini kutokana na umbali wake inasababisha waharibu miundombinu inayokwenda kwa wananchi wengine. Niombe RUWASA msogeze huduma kwao na mtoe elimu ili wawe mabalozi wenu wazuri katika kulinda miundombinu hiyo,” alisema Diwani Mkinyaga.

Nao baadhi ya wananchi akiwemo Kelosi Mponda kutoka Kijiji cha Makatapola ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa kusogeza huduma hiyo ya maji katika kijiji hicho ambacho kwa n zaidi ya miaka 60 ya Uhuru hakikuwa na huduma hiyo.

“Tulikuwa tunatembea zaidi ya kilometa saba kufuata maji mtoni, maji hayo hayakuwa safi na salama yalikuwa, ni neema ya Mungu tu ilitukinga na magonjwa, lakini kwasasa tunakunywa maji kama wanayokunywa mjini-hata ngozi zetu zinatakata siku hizi,” alisema Kelosi.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button