Sh bilioni 22 zatumika ujenzi kituo cha kupima magari

MENEJA wa Wakala ya Barabara nchini (TANROADS) Mkoa wa Mara, Mhandisi Vedastus Maribe amesema zaidi ya Sh billioni 22 zimetumia katika ujenzi kituo cha kupimia magari (mizani) cha kisasa katika eneo la Rubana Wilaya ya Bunda.
Mhandisi Maribe alisema hayo Novemba 8, 2023 alipozungumza na baadhi ya waandishi wa habari kutoka Kanda ya Ziwa kwenye ziara ya kutembelea miradi mbalimbali ya matengenezo inayotekelezwa serikali.

Alisema kulikuwa na vituo viwili vya Silali na Rubana ambavyo ni vidogo lakini kinachojengwa nitakuwa kikubwa cha kisasa chenye uwezo wa kupima huku gari likiwa kwenye mwendo.
Mhandisi Maribe alisema ujenzi huo fedha zote zimetolewa na serikali na mhandisi mshauri ni Kampuni ya Norplan (T) Ltd na ujenzi ulianza Januari 2022 na utakamilika Novemba 2023 kwa sasa umefikia asilimia 85 na mkandarasi kutoka kampuni ya (CHICO).

“Lengo serikali kujenga mizani hiyo sio kukusanya mapato bali ni kuthibiti uzito kwenye magari na kutoa adhabu ya faini wakatao kaidi kwani moja ya changamoto inayoharibu barabara ni uzito uliopitiliza katika gari.”alisema mhandisi Maribe.
Kaimu meneja wa mawasiliano na uhusiano kutoka Tanroads makao makuu, Aisha Malima alisema wameamua kushirikiana waandishi wa habari ili kuweza kuitangaza miradi mbalimbali ya kimkakati inayotekelezwa na fedha za serikali kwa lengo la kukuza uchumi.

Mhandisi mshauri kutoka kampuni ya Norplan mhandisi, George Mwandiga alisema mizani hiyo itakuwa niya kwanza kwa ukubwa na ubora ambapo Itapunguza msongamano wa magari yanayosubiri kupima kwenye mizani huo.
Mhandisi Mwandiga alisema umebakia ujenzi wa njia mbili na ukamilishaji wa maegesho ya gari kama gari likipata hitilafu wakati likiwa kwenye kituo hicho.


