Watanzania wahitimu China watakiwa kuwa mabalozi wa nchi

CHINA: Balozi wa Tanzania nchini China, Dk. Suleiman Haji Suleiman, amewataka Watanzania wanaohitimu masomo yao katika vyuo mbalimbali nchini humo mwaka 2026, kuwa mabalozi wazuri wa Tanzania kwa kutumia maarifa, ujuzi na uzoefu walioupata katika kujiletea maendeleo binafsi na kuchangia maendeleo ya taifa wanaporejea nyumbani.

Balozi Dk. Suleiman ametoa wito huo wakati wa hafla maalumu ya kuwaaga wanafunzi wa Kitanzania wanaomaliza masomo yao nchini humo iliyoandaliwa na Ubalozi wa Tanzania kwa lengo la kuwapongeza na kuwapa nasaha kuhusu maisha baada ya kuhitimu.

“Ni muhimu kwenu kama vijana kutumia elimu mliyoipata kama nyenzo ya kuleta mabadiliko chanya katika jamii, kuibua na kutumia fursa za kiuchumi zilizopo nyumbani, pamoja na kuendelea kuitangaza vyema nchi yenu katika maeneo yote mtakayokuwa mkiyahudumia.

“Pamoja na mambo mengine, mnarejea nyumbani mkiwa mmebeba maarifa, ujuzi na uzoefu wa kimataifa. Ni wajibu wenu kuwa mabalozi wazuri wa Tanzania, kuishi katika maadili mema, kufanya kazi kwa bidii na kutumia elimu yenu kuleta maendeleo kwa taifa letu,” alisema.

Aidha, Balozi Dk. Suleiman ameahidi kutatua changamoto za wanafunzi wanaosoma nchini China kama vile; bima ya afya, vibali vya ukaazi na upatikanaji wa nafasi za mafunzo kwa vitendo ndani na nje ya China.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Wanafunzi wa Tanzania Beijing, Avitus Barnabas ameishukuru Ofisi ya Ubalozi kwa kuwafanyia hafla hiyo pamoja na nasaha kutoka kwa Balozi Dk. Suleima ambapo amesema ni heshima kubwa kupata nafasi ikiwamo ahadi ya Balozi kutatua baadhi ya changamoto wanazokumbana nazo wanafunzi wanaosoma nchini humo.

Hafla hiyo imehudhuriwa na wanafunzi 150 waliohitimu katika ngazi za Shahada ya Kwanza, Shahada ya Uzamili na Shahada ya Uzamivu katika fani mbalimbali ikiwemo Sayansi, Teknolojia, Tiba, Uhandisi wa Miundombinu, Mafuta na Gesi, Madini na Nishati ya Umeme na wageni kutoka nchi za Mauritania, Gambia, Congo, Kenya, Uganda, Namibia, Ufaransa, Morocco pamoja na wenyeji wao China.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button