Trump kuzuia kufungwa TikTok Marekani

MAREKANI : RAIS mteule wa Marekani, Donald Trump, atafanya juhudi kuzuia kufungwa kwa TikTok kabla ya marufuku dhidi ya programu hiyo kuanza kutekelezwa wikiendi hii.
Mbunge Mike Waltz wa Florida alisema Trump atachukua hatua iwapo Mahakama Kuu itaendelea na sheria ya kupiga marufuku TikTok nchini Marekani, isipokuwa kampuni ya ByteDance iuze jukwaa hilo kabla ya tarehe 19 Januari.
Katika wiki ya mwisho ya utawala wa Rais Biden, pia kuna juhudi za kutafuta njia za kuzuia TikTok kutoweka ghafla. Mmiliki wa TikTok kutoka China, ByteDance, amesema inajiandaa kuzima programu hiyo kwa watumiaji milioni 170 wa Marekani ifikapo Jumapili.
“Tutachukua hatua stahiki ili kuzuia TikTok isifungwe,” alisema Waltz Alhamisi. Aliongeza kuwa sheria inaruhusu kuongeza muda wa siku 90 kwa ByteDance ikiwa hatua kubwa itachukuliwa kuelekea kuuzwa kwa jukwaa hilo. SOMA: Biden kusaini sheria marufuku ya Tiktok Marekani
“Kimsingi, hilo litampa Rais Trump muda ili TikTok iendelee kufanya kazi,” alisema.
Hata hivyo, haijulikani kama hatua hiyo inaweza kukwepa sheria iliyopitishwa na Congress. Programu hiyo imepigwa marufuku kwa misingi ya usalama wa taifa kutokana na wasiwasi kuhusu ukusanyaji wa data na Chama cha Kikomunisti cha China.



