Kilosa: Kabudi amwaga wapinzani kwa 76%

MOROGORO : ALIYEKUWA Waziri wa Habari, Utamaduni ,Sanaa na Michezo, Profesa Palamagamba Kabudi ameibuka mshindi wa kura za maoni katika Jimbo la Kilosa kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Profesa Kabudi ameongoza kwa kishindo baada ya kupata kura 9,102, sawa na asilimia 76.57 ya kura zote zilizopigwa 11,887 na kuwashinda wenzake wanne waliokuwepo katika kinyang’anyiro hicho. SOMA: Wajumbe wameamua
Kwa mujibu wa Katibu wa CCM wilaya ya Kilosa ,Janus Mfaume alimtaja kuwa Profesa Kabundi amepata kura hizo na kuongoza dhidi ya wanne waliowania nafasi hiyo ambapo kura zao na asilimia zao katika mabano ni pamoja na Dk Ford Moses Chisongela aliyepata kura 854 (7.18).
Wagombea wengine ni Menance Thomas Mhombwe aliyepata kura 830 (6.98),Ahmed Mustafa Mkulo aliyepata kura 661 (5.56), Dotto Said Ndumbikwa kura 323 (2.71) na Rehema Athuman Simba aliyepata kura 117 (0.98).
Matokeo haya yanaonesha uungwaji mkono mkubwa kwa Profesa Kabudi kutoka kwa wanachama wa CCM, hivyo kumuweka kwenye nafasi nzuri kuelekea uchaguzi mkuu iwapo jina lake litapitishwa kupeperusha bendera ya chama hicho.



