Macron amteua Lecornu Waziri Mkuu mpya

PARIS, UFARANSA : RAIS wa Ufaransa, Emmanuel Macron, amemteua Waziri wa Ulinzi na mshirika wake wa karibu, Sebastien Lecornu, kuwa Waziri Mkuu mpya, hatua inayolenga kupunguza mzozo wa kisiasa unaoendelea nchini humo.

Lecornu mwenye umri wa miaka 39, anachukua nafasi ya Francois Bayrou na kuwa Waziri Mkuu wa saba chini ya uongozi wa Macron. Kwa mujibu wa Ikulu ya Elysee, Rais Macron alimchagua Lecornu kutokana na ukaribu wake wa kisiasa na uaminifu wa muda mrefu, badala ya kujaribu kutanua wigo wa kisiasa wa serikali yake.

Hatua hiyo inakuja wakati ambapo maandamano makubwa yanatarajiwa kufanyika siku chache zijazo, yakionesha shinikizo kubwa la kisiasa na kijamii linalomkabili kiongozi huyo. SOMA: Bayrou aondoka, Macron aanza mchakato kumtafuta mrithi

Katika hatua nyingine, Rais Macron amemtaka Lecornu kuanza mashauriano na makundi mbalimbali ya kisiasa yaliyoko bungeni ili kufanikisha kupitishwa kwa bajeti ya taifa na kuhakikisha makubaliano muhimu kwa miezi ijayo. Kuteuliwa kwa Lecornu, anayejulikana kwa msimamo wake thabiti na uaminifu kwa Rais Macron, kunatazamwa kama ishara ya Rais kutegemea zaidi washirika wake wa karibu katika kipindi hiki kigumu.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button