Daraja kuondoa shida ya mafuriko Ngara

NGARA, Kagera: Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) wametekeleza mradi wa ujenzi wa daraja la mawe na saruji ambao umefikia asilimia 95.
Kukamilika kwa daraja hilo kutapunguza changamoto ya mafuriko kwa wananchi wa Kata ya Mubumba na Bukiriro wilayani Ngara mkoani Kagera.
Meneja wa TARURA Wilaya ya Ngara, Makoro Magori amesema mradi huo umegharimu Sh milioni 736.3 kupitia Mpango wa Serikali wa Kupunguza Vikwazo unaofadhiliwa na Benki ya Dunia.

Amesema daraja hilo ambalo limeokoa gharama za serikali kwa asilimia 33 huku wananchi wa kata hizo wakipunguza Mzunguko kutoka kilometa 23 hadi kilometa 10 na kupata mawasiliano ya uhakika ya kudumu.
Kiongozi wa Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Ismail Ussi amewapongeza TARURA kwa uwezo mkubwa wa utekelezaji wa Mradi huo na kuokoa maisha ya wananchi ambao wamekuwa wakipitia changamoto ya mawasiliano
Alitoa wito kwa wananchi wa Ngara na kata hizo kutumia fursa ya uwepo wa daraja kuzalisha kwa wingi mazao kutafuta masoko kufanya kazi kwa bidii na kuunga mkono juhudi za serikali.



