Kanisa Katoliki Mafinga latoa kauli kuhusu Padre Kibiki

IRINGA: Kanisa Katoliki Jimbo la Mafinga limetoa ufafanuzi kuhusu sintofahamu iliyozuka juu ya Padre Jordan Kibiki, aliyeripotiwa kujiteka wiki iliyopita, na kufafanua kuwa kilichotokea ni matokeo ya tatizo la afya ya akili.

Taarifa iliyotolewa na kanisa hilo inaonesha Jeshi la Polisi limemwachia huru baada ya uchunguzi kubaini ukweli huo.

Akizungumza na waandishi wa habari, Askofu wa Jimbo la Mafinga, Vicent Mwagala, alisema Padre Kibiki, ambaye ni Mkurugenzi wa Kituo cha Afya Nyololo na Paroko Msaidizi wa Parokia hiyo, alitarajiwa Septemba 18, 2025 kuhudhuria kikao cha afya katika ofisi za Halmashauri ya Mufindi, lakini hakuwasili licha ya kuondoka nyumbani mapema asubuhi.

Kwa mujibu wa Askofu Mwagala, taarifa za kutoweka kwake zilitolewa baada ya Padre Isaac Nzigilwa, Paroko wa Nyololo, kuona gari la Padre Kibiki limeegeshwa barabarani bila dereva na kushindwa kumpata kwa simu.

“Ndipo jitihada za kumtafuta zikaanza mara moja,” alisema.

Alisema Padre Kibiki alikuwa kwenye hali ya msongo wa mawazo na Polisi walipomhoji, alikiri kujitenga kutokana na shinikizo la kifedha baada ya kupoteza fedha alizokopa katika biashara ya mtandao (online business scam), jambo lililomwingiza katika huzuni na hofu kubwa.

“Baada ya uchunguzi wa kitabibu, madaktari walithibitisha kuwa Padre Kibiki alikuwa anakabiliwa na msongo wa mawazo (depression). Kwa ushauri wa wataalamu, alipelekwa Hospitali ya Rufaa ya Tosamaganga kwa matibabu na uangalizi wa karibu wa afya ya akili,” alibainisha Askofu Mwagala.

Alisema Jeshi la Polisi Mkoa wa Iringa liliidhinisha kufutwa kwa tuhuma zote na kumwachia huru mwishoni mwa Septemba 2025, baada ya kuridhishwa na vielelezo vya kitabibu na maelezo ya Kanisa.

Askofu Mwagala aliongeza kuwa Jimbo la Mafinga linaendelea kufuatilia afya ya Padre Kibiki ili aweze kurejea katika hali ya kawaida na kuendelea na majukumu yake ya kiroho.

“Tunawaomba waumini na jamii kwa ujumla kuendelea kumwombea Padre Jordan ili apone haraka. Tunashukuru pia vyombo vya habari kwa ushirikiano wao katika kipindi hiki kigumu,” alisema Askofu Mwagala.

Kwa mujibu wa wataalamu wa afya ya akili, msongo wa mawazo ni miongoni mwa changamoto kubwa za kiafya zinazokabili watu wa rika na nafasi mbalimbali, ikiwemo viongozi wa dini (Shirika la Afya Duniani – WHO, 2023).

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button