Mwinyi kuboresha bandari ya Shumba

PEMBA : MGOMBEA Urais wa Zanzibar kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM) Dk. Hussein Ali Mwinyi ameahidi kuendelea kuboresha miundombinu ya bandari ya Shumba kisiwani Pemba ili kupunguza gharama za maisha na bei za vyakula ambazo zimekuwa zikiwakabili wananchi kwa muda mrefu.

Amesema, serikali inaendelea kuimarisha bandari hiyo na katika kipindi kifupi kijacho bandari hiyo itakuwa ni bandari kuu kwa mkoa wa Kaskazini Pemba ambapo meli kubwa za nje zitaweza kufunga gati moja kwa moja.

Hayo aliyabainisha wakati akizungumza na wananchi wa Jimbo la Konde huko katika mkutano wake wa kampeni za Urais katika kijiji cha Msuka, Wilaya ya Micheweni mkoa wa Kaskazini Pemba. Ameeleza kuwa maboresho ya bandari yataongeza ufanisi wa upokeaji wa mizigo na bidhaa kutoka Tanzania Bara na Nje ya Nchi jambo litakalosaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza gharama za chakula kisiwani Pemba.

Aidha amesema kuwa uboreshaji wa bandari hiyo ni hatua muhimu ya kupunguza gharama za usafirishaji wa bidhaa muhimu, hatua ambayo itapelekea kushuka kwa bei za vyakula na bidhaa nyingine zinazotegemewa na wananchi wa kisiwa hicho. “Tunatambua changamoto kubwa ya gharama za usafirishaji wa bidhaa kutoka Unguja kuja Pemba, ambayo inachangia kupanda kwa bei za vyakula na bidhaa nyingine muhimu kupitia bandari ya Shumba tutahakikisha huduma bora zinapatikana kwa gharama nafuu,” Dk. Mwinyi.

Amesema, serikali imejidhatiti katika kujenga na kuboresha bandari na kueleza kuwa katika kipindi cha miaka mitano ijayo serikali itaijenga bandari ya Wete ili iwe bandari ya Kimataifa. “Katika miundombinu mikuu ya nchi ni bandari, barabara na viwanja vya ndege, barabara zinajengwa, bandari ndo kama hizi na uwanja wa ndege wa Pemba tayari mkandarasi yupo na anaanza kazi ya ujenzi wa kiwanja cha ndege cha Pemba cha kimataifa,”alisema

Vile vile, Dk. Mwinyi ameeleza kuwa Serikali ina mpango wa kujenga maghala maalum ya kuhifadhia chakula, ili wakati wa msimu wa mavuno bara, basi Zanzibar iweze kununua chakula kwa wingi na bei nafuu kisha kuhifadhi kwa matumizi ya muda mrefu.

Hivyo ameagiza mamlaka husika kusimamia utekelezaji wa mikakati hiyo kwa ufanisi huku akisisitiza kuwa hatua hizo zitasaidia kuimarisha uchumi wa wananchi wa Pemba na kuhakikisha upatikanaji wa chakula kwa bei nafuu muda wote.

Dk. Mwinyi amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kusimamia miradi ya maendeleo inayogusa maisha ya wananchi moja kwa moja, ikiwemo ujenzi wa miundombinu bora ya bandari, barabara, afya na elimu.

Akizungumzia changamoto ya ajira alisema serikali haitashindwa kulivalia njuga changamoto ya ajira kwa vijana ili kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla. Amesema kuwa, Ilani ya chama cha Mapinduzi CCM ya mwaka 2025/2030 imedhamiria kutoa ajira kwa vijana zipatazo 350,000, hivyo watahakikisha wanavuka lengo hilo ili kuona kwamba kila mmoja anapata kipato cha kujikwamua kimaisha.

“Kipindi kilichopita tuliahidi ajira laki tatu lakini tumeajiri vijana 275,000, hivyo basi Ilani yetu ya mwaka 2025/2030 tutatoa ajira kwa vijana 350,000, ingawa awamu hii tunataka tuvuke lengo, ili vijana wote wanufaike,” alieleza Dk. Mwinyi.

Dk. Mwinyi amesema suala la ajira kwa vijana ni changamoto kubwa, ingawa serikali inajitahidi kuweka mazingira rafiki kwa kuwapatia mikopo isiyo na riba itakayowawezesha kujikwamua kiuchumi. SOMA: Mwinyi azidi kuhimiza amani

Dk. Mwinyi akizungumzia maendeleo yaliyopatikana katika miaka mitano iliyomalizika alisema serikali imefanya vizuri katika sekta ya elimu, barabara, maji na afya na kuahidi kuwa itaendelea kujenga hospitali za mikoa na vituo vya afya Ili kuhakikisha mikoa yote inajitegemea kiafya na kutoa huduma bora katika maeneo yao.

Ameahidi kuwa ataendelea kuimarisha ustawi wa jamii na kuyawezesha makundi yote ili yaweze kujikwamua kiuchumi. Amewasisitiza wananchi kuendeleza amani, umoja na mshikamano ili nchi iendelee kupiga hatua za kimaendeleo na kuwaomba kukichagua Chama cha Mapinduzi kiendelee kuwatumikia.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button