HESLB, NCAA kushirikiana kugharamia wanafunzi

ARUSHA: BODI ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) wamesaini makubaliano kugharamia masomo ya wanafunzi wanaotoka kwenye familia za kipato cha chini katika eneo la Hifadhi ya Ngorongoro ikiwa ni mikakati ya bodi hiyo kuinuwa viwango vya elimu.

Makubaliano hayo yalifanyika jijini Arusha na wakuu wa taasisi hizo mbili na malengo makuu ni kuanzisha na kushirikiana na kuratibu na kugharamia wanafunzi wenye sifa kutoka katika kaya za kipato cha chini wanaoishi katika eneo la Hifadhi ya Ngorongoro.

Kamishina wa Uhifadhi wa NCAA, Abdul-Razaq Badru alisema mamlaka hiyo imeanzisha mfuko huo maalumu kwa ajili ya wanafunzi wa eneo la hifadhi hiyo ambao watapata udahili katika maeneo ya program za kipaumbele cha hifadhi hiyo yenye hadhi kubwa duniani

‘’Tunaanzisha mfuko maalumu kwa ajili ya kutoa ufadhili mahsusi katika maeneo mahsusi ambayo  ni Sayansi ya Anga ,menejimenti ya malikale (Natural Hertage/Archeology )na uhifadhi wa wanyama Pori (Wildlife Management),’’alisema Kamishina Badru.

Alisema kuwa NCAA siyo wataalamu hivyo wameamua kushirikiana na HESLB na katika mwaka huu 2025/26 mamlaka hiyo itaanza kugharamia wanafunzi 50 kwa kushirikiana na jamii ya maeneo ya uhifadhi ya Ngorongoro ili kuongeza wanafunzi wenye sifa stahiki watakaosoma, kuhitimu na kuchagiza ustawi wa jamii na maendeleo ya uchumi wa eneo hilo la hifadhi.

Naye, Mkurugenzi Mtendaji HESLB, Dk Bill Kiwia amesema kuwa hatua ya HESLB na NCAA kuingia katika ushirikiano rasmi ni sehemu ya utekelezaji wa dhima ya serikali kuzitaka taasisi za umma kushirikiana kutoa huduma bora kwa wananchi na ametoa wito kwa taasisi nyingine za umma na binafsi kushirikiana na bodi yake kuwahudumia wananchi kwa ufanisi zaidi kwa kuwa taasisi yake ina ujuzi na udhoefu mkubwa na kusimamia upangaji na utoaji wa mikopo ya wanafunzi kwa zaidi ya miaka miwili.

‘’Hatua hii ya kusaini makubaliano kati ya taasisi zetu iwe ni chachu kwa taasisi mbalimbali za umma na binafsi kushirikiana na HESLB katika kusaidia na kugharamia masomo ya vijana wa kitanzania kwani sisi tuna ujuzi na,uzoefu na mifumo ya kuchakata taarifa za wanafunzi kwa ufanisi’’alisema Dk Kiwia.

Halfa hiyo ilihudhuriwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya NCAA, Mkuu wa Majeshi wa Mstaafu ,Venance Mabeyo ambaye ni Mwenyekiti wa Bodi ya NCAA na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya HESLB, Profesa Hamis Dihenga ambao kila mmoja waliunga mkono hatua hiyo ya kihistoria iliyofikiwa na taasisi hizo ikilenga kuinua maslahi ya wananchi wa Ngorongoro.

Mbeyo alisema anashukuru kushuhudia makubaliano hayo mazuri na yenye utaratibu mzuri unaoeleweka wa kugharamia wanafunzi wa jamii yenye kipato cha chini Ngorongoro kwani hali hiyo inaweza kuondoa migogoro katika eneo hilo kwa kuwa kutakuwa na jamii yenye uelewa mkubwa wa uhifadhi na hifadhi itadumu na serikali inahitaji hifadhi hiyo kwa moja ya chanzo kikuu cha mapato ya taifa.

Prof Dihenga alisema aliungana na Mwenyekiti mwenza wa NCAA na kusema kuwa ushirikiano huo ni sehemu ya kushiriki kwa vitendo katika nia thabiti ya serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan ambayo imeweka msisitizo mkubwa katika elimu na hata utoaji wa mikopo ya elimu ya kati ni kwa maono yake Rais na kila mwaka serikali imekuwa ikiongeza kiasi kikubwa cha fedha za mikopo kwa wanafunzi lakini mahitaji ni makubwa.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button