Mwigulu aagiza Watanzania wapewe kandarasi
SERIKALI imeagiza wakandarasi wazawa wapewe kazi za ujenzi wa miradi ya barabara.
Waziri Mkuu, Dk Mwigulu Nchemba ametoa agizo hilo alipozungumza na wakazi wa Dar es Salaam katika mkutano wa hadhara katika Kata ya Mbezi wilayani Ubungo mkoani humo.
Dk Mwigulu alisema wakandarasi wazawa hawaaminiwi ndio maana hawapewi kazi huku akisisitiza kuwa haipendezi kuona barabara mpaka za mitaani za umbali mfupi wa kilometa moja zote wamepewa wageni.
SOMA: Latra kutoa vibali maalumu mabasi 150 Dar
“Miaka zaidi ya 60 ya Uhuru lazima tuwaamini wakandarasi wazawa kwa sababu hii ni nchi yao hivyo watakuwa wakitekeleza kazi wakijua kuwa wanaifanyia kazi nchi yao. Tanzania ni nchi yao hivyo msiogope kuwapa kazi wafanye,” aliongeza.
Alisema utaratibu huo utasaidia wakandarasi wazawa kuwasimamia wengine wote wanaotoka nje ya nchi na kuwapa kazi kama ilivyokuwa awali Watanzania ndio waliokuwa wakipewa mikataba na wageni.
“Na kazi kubwa zinafanywa na wazawa, hawa wageni wanatembea na mikoba yao tu huku akisisitiza kuwa wakandarasi wengine wanalipwa na serikali huku wakiwababaisha wakandarasi wazawa,” alisema Dk Mwigulu.
Alisema katika eneo la ajira hakuna nchi yoyote duniani wananchi wake wote wameajiriwa serikalini na kwamba ikiwa serikali itawajengea uwezo wazawa nao watawaajiri vijana wa Kitanzania wanaohitimu ujuzi mbalimbali.
“Na hili liende sambamba na maeneo mengine, kwamba kazi inayoweza kufanywa na Mtanzania ifanywe na Mtanzania kwa sababu nchi hii Watanzania ni yao. Yapitiwe hadi maeneo ya biashara, ambazo zinaweza kufanywa na Watanzania zifanywe na Watanzania,” aliongeza Dk Nchemba.
Dk Mwigulu aliielekeza idara inayohusika ipitie upya kwenye kazi na kwenye biashara na maeneo yote ambayo walishatoa leseni na yale wanayoendelea kutoa leseni ili maeneo ambayo kazi inaweza kufanywa na Mtanzania ifanywe na Mtanzania.
Alisema hakuna haja ya kuogopa kuwa ataharibu kwa sababu akiharibu anafukuzwa mara moja na kwamba watumishi wazembe, wavivu na wala rushwa wasihamishwe bali wafukuzwe kwa sababu kuna vijana wengi wenye uwezo wa kutekeleza mambo hayo.



