Watanzania wasikubali kutumika kuvuruga amani, rasilimali

WATANZANIA tutaendelea kuwakumbusha kuwa amani ni urithi mkubwa ambao taifa letu linahitaji kuendelea kuutunza kwa ajili ya vizazi na vizazi.

Lazima kila mwananchi atambue kuwa amani ni rasilimali isiyoonekana kwa macho, lakini yenye thamani inayozidi madini, gesi au ardhi.

Kama ambavyo viongozi wakuu wakiongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan wameendelea kusisitiza umuhimu wa kujitambua na kuithamini amani hiyo, ndivyo nasi tumeendelea kulisisitiza hilo.

Tunapenda kuwakumbusha Watanzania namna siku zote wameweza kuishi kwa mshikamano, kufanya kazi kwa uhuru na kujenga uchumi unaoendelea hatua kwa hatua, basi waendelee kuenzi mshikamano huo.

Rai yetu ni kwa Watanzania kukukataa kutumika na baadhi ya watu walioko ndani na nje ya nchi, wanaojaribu kuigawa jamii na kututumia kama nyenzo ya kuvuruga utulivu wetu.

Katika nyakati hizi za ushindani wa kisiasa, migogoro ya kijamii, au tofauti za kimtazamo, mara nyingi hutokea mashinikizo ya makusudi ya kuhamasisha chuki, kueneza taarifa potofu au kuchochea makundi fulani dhidi ya mengine.

Changamoto kubwa pia imekuwa matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii ambayo imegeuka kuwa chombo kinachoweza kutumiwa vibaya na wenye nia ovu.

Ni ukweli usipingika kama Watanzania wataacha ama kukokosa uzalendo ni rahisi kuingia katika mtego wa kugawanywa bila hata kutambua. Lakini ukweli ni kuwa jukumu la kuilinda amani ya Tanzania lipo mikononi mwa kila mmoja wetu.

Tusikubali kutumiwa kuanzisha vurugu au misukosuko inayoweza kulisababisha taifa kupata majeraha ya muda mrefu. Historia inatuonesha kuwa pale amani inapopotea, kuirudisha kunahitaji gharama kubwa kuanzia kiuchumi, kijamii na hata kisaikolojia.

Labda tukumbushe tu hakuna mahali vurugu zimewahi kutoa hazitoi majibu au suluhisho, zaidi zinabomoa wala chuki haijawaji kutengeneza mustakabali zaidi ya kuharibu.

Wito wetu kwa Watanzani ni kuhakikisha kipindi hiki wanasimama kidete na kusema hapana, hapana kwa uchochezi, hapana kueneza taarifa zisizothibitishwa, hapana kutumiwa kama vibaraka wa maslahi binafsi ya watu wachache.

Huu ni wakati wa kuonesha ukomavu kama taifa kuisimamia sifa yake kama kisiwa cha amani kwa kuchagua majadiliano, busara, na uzalendo.

Tuendelee kuulinda huu msingi wetu wa thamani kubwa yaani amani, kwa sababu bila amani, hakuna maendeleo, hakuna umoja na hakuna Tanzania tunayoitamani.

Tulinde amani yetu, rasilimali zetu na urithi mkubwa wa rasilimali tulizonazo kwa maslahi ya taifa, na kukataa kutumika kuharibu kwa kuwafurahisha wachache wasiotamani kuiona Tanzania yenye maendeleo ya kasi na makubwa.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button