Zanzibar kutokomeza malaria ifikapo 2030

MKURUGENZI wa Kinga na Elimu ya Afya Dk Salim Slim amesema Wizara ya Afya  Zanzibar imekusudia kumaliza malaria Zanzibar ifikapo mwaka 2030.

Akifungua kikao kazi kilichoandaliwa na kitengo cha kumaliza malaria Zanzibar kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo, Dk Slim amesema mradi wa kumaliza malaria Zanzibar umeendelea kuleta mafaniko katika kupunguza maambukizi na athari za ugonjwa huo hususani kwa watoto na wazee.

“Kupungua kwa maambukizi ya malaria kumeanza kuleta faraja kubwa Zanzibar ikiwa ni ishara kwamba visiwa hivi vinaweza kurejea katika ustawi wa kijamii na kiuchumi na kuifanya Zanzibar kuendelea kupiga hatua kubwa katika maendeleo ya sekta ya utalii,” alisema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mradi wa Kumaliza Malaria Zanzibar (MEZA), Richard Silumbe amesema  mradi huo unaotekelezwa kwa ufadhili wa Shirika la Gates na wadau wengine unaendelea kushirikisha sekta mbalimbali ili kuhakikisha Wazanzibari wanakuwa salama.

Silumbe amesema mradi huo ulioanza mwaka mmoja uliopita unalenga kuimarisha utekelezaji wa majukumu ya programu ya kumaliza malaria, hususani katika ngazi za wilaya na kuwafikia walengwa. “Utekelezaji wa mradi huu unakusudia kuunganisha nguvu kutoka sekta za utalii, maji, mipango miji na taasisi nyingine muhimu, ili kuongeza ushirikiano na kuimarisha mikakati ya kupunguza na kumaliza maambukizi ya malaria Unguja na Pemba,” alisema.

Silumbe amesema kikao hicho kimelenga kuwakutanisha wadau na kujadili mikakati ya kitaalamu itakayosaidia kuondoa kabisa ugonjwa wa malaria Zanzibar. Naye Kiongozi wa kitengo cha kumaliza malaria Zanzibar, Shija Joseph Shija alisema serikali kupitia programu ya kupambana na malaria imegawa zaidi ya vyandarua 90,000 kwa wananchi wa Unguja na Pemba.

Shija amesema hivi sasa ugawaji wa vyandarua unaendelea kwa wajawazito na watoto wadogo kupitia vituo vya afya wanapotembelea kliniki kwa ajili ya vipimo na huduma nyingine za afya ya mama na mtoto. “Kitengo kinaendelea na zoezi la upulizaji wa dawa katika maeneo yenye idadi kubwa ya maambukizi ya malaria, na tunaendelea na zoezi la kuwafanyia vipimo wananchi katika maeneo ambayo idadi ya wagonjwa wanaendelea kuathirika,” alisema.

SOMA: Maambukizi ya malaria yapungua asilimia 6.7

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button