Atlas Marathon na mikakati ya kutokomeza Ukatili dhidi ya Watoto

DAR ES SALAAM: Waaandaji wa Atlas half Marathon 2023, wamesema mbio hizo kwa mwaka huu zinalenga kupeleka ujumbe wa kupinga na kutokomeza ukatili dhidi ya watoto kwenye jamii.
Akizungumza wakati wakutambulisha zawadi hizo kwa washindi mbalimbali, Mwalimu kutoka Shule ya Atlas, Willbroad Prosper amesema kuwa Atlas Half Marathon ina kauli mbiu isemayo, “Tokomeza Ukatili dhidi ya Watoto” ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuwalinda watoto dhidi ya ukatili.
Amesema kutakuwa na zawadi kwa mshindi wa kwanza mpaka mshindi watano kwa jinsia zote watakao shiriki kuanzia kilomita 10 na kilomita 21. Pia kutakuwa na zawadi maalumu kwa watoto jinsia zote kuanzia mshindi wa kwanza hadi watano watakao shiriki mbio za kilomita 5.
Prosper amesema kuwa Marathon ya mwaka huu imeboreshwa zaidi kwani wana vifaa vizuri kwaajili ya washiriki huku wakiwa na lengo la kutokomeza ukatili katika jamii hasa watoto.
Kwa upande wake Katibu wa Chama Cha riadha Tanzania, Samwel Mwela amesema kuwa maandalizi yote yamekamilika hivyo wananchi na wadau wote wajitokeze katika kushiriki mbio hizo zitakayofanyika kesho Oktoba 14, 2023 kuanzia saa kumi na moja mpaka saa 4 asubuhi kuanzia njia ya Goba Madale katika shule ya Atlas Madale kwa msimu wa tano mfululizo.



