Azam FC yajipanga dhidi ya KMKM

KUELEKEA mchezo muhimu wa Kombe la Shirikisho Afrika, klabu ya Azam imerejea katika mazoezi makali huku ikitamba kuwa iko tayari kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania dhidi ya KMKM ya Zanzibar.

Akizungumza na DailyNews Digital Dar es Salaam, Ofisa Habari wa Azam, Hasheem Ibwe, amesema maandalizi ya timu hiyo yanaendelea vizuri licha ya kuwepo kwa baadhi ya wachezaji ambao wanakosekana kwa sababu mbalimbali.

“Ni mechi ngumu sana kwa sababu kila timu inatafuta namna ya kuifanya nchi yake ijivunie. Lakini sisi tunaamini kuwa timu yoyote itakayovuka kati ya KMKM na Azam, basi Tanzania ndio itakayokuwa imevuka,” amesema Ibwe.

Ameongeza kuwa maandalizi ya mchezo huo ni sehemu ya dhamira ya klabu hiyo ya kuhakikisha kuwa Tanzania inaendelea kuwa na heshima katika mashindano ya kimataifa.

“Tunaendelea na mazoezi kujiandaa na mchezo wa Kombe la Shirikisho Afrika. Kama viongozi tumejiandaa. Ni kiu ya mashabiki kuona tunafanya vizuri, na sisi tunapambana kuhakikisha tunafanikisha hilo,” ameongeza.

Ibwe amesema kuwa mchezo huo si tu wa klabu, bali ni wa taifa zima kwani Azam inabeba matumaini ya Watanzania katika ngazi ya kimataifa.

Kwa sasa, kikosi cha Azam kipo kambini kikiendelea na maandalizi ya mwisho kabla ya kuivaa KMKM katika mchezo huo mtoano wa Kombe la Shirikisho Afrika Oktoba 18 kisha marudiano Oktoba 25, ambapo matokeo ya jumla yatatoa mwakilishi mmoja wa Tanzania katika hatua inayofuata.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button