Hospitali Haydom kinara uzazi salama

Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali ya Kilutheli Haydom, iliyoko wilayani Mbulu mkoa wa Manyara ambaye pia ni kiongozi wa mradi wa kitita cha uzazi salama (SBBC),Daktari Paschal Mdoe amesema hospitali hiyo ndiyo inayoongoza utekelezaji wa miradi katika mikoa mitano na vituo vya kutolea huduma za afya 142 katika awamu ya pili ya mradi.
Katika utekelezaji wa kitita cha uzazi salama (SBBC) awamu ya kwanza amesema utekelezaji wa mradi ulikuwa katika hospitali 30 katika mikoa mitano yenye uwiano wa hospitali 6 kila mkoa na kuleta matokeo chanya ambapo katika akina mama mia moja waliokuwa wanafariki kabla ya utekelezaji wa mradi kumekuwepo na upungufu wa vifo vya akina mama 75.

”Akina mama mia moja ambao walikuwa wapoteze maisha kwenye hizo hospitali, akina mama 25 ndio waliokuwa wanapoteza maisha na 75 ndio waliokuwa wanaokolewa,” amesema Mdoe.
Alibainisha kuwa baadhi ya hospitali kwa watoto wachanga ambao walikuwa wanafariki dunia mara baada ya kuzaliwa idadi yao pia imepungua.
”Wastani wa watoto mia moja ambao waliokuwa wapoteze maisha kabla ya mradi baada ya utekelezaji wa mradi huu tumeona tumepunguza kwa zaidi ya asilimia 50 ya wale watoto wachanga ambao walikuwa wanafariki”

Hatua hiyo amesemani kubwa badala ya kupoteza maisha kwa watoto mia moja wanafariki watoto wachanga kati ya 50 na 60 ni matokeo chanya ya mradi na kulazimika serikali kuiendesha kwa ubia katika hospitali 142.
Mwaka huu ni wa pili wa utekelezaji wahudumu wa afya wamehamasika kutoa huduma kwa ukamilifu,kujifunza kwa kasi lengo ni kuongeza ubora wa utoaji huduma kwa akina màma wanaokwenda katika hospitali za mradi na kupungua kwa vifo vya watoto wachanga na akina mama.
Naye rais wa chama cha wakunga Tanzania (Tanzania Midwives Associations-TAMA) Daktari Beatrice Mwilike amesema kuwa wakunga wamekuwa mstari wa mbele katika kutoa huduma za uzazi na kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi.
Ukienda katika vituo vya kutolea huduma mtoa huduma wa kwanza ni mkunga na pia ndiye anayepokea mtoto mchanga anapozaliwa.
Kwa kushirikiana na mradi wa SBBC mafunzo kwa wakunga wanaofanya kazi katika mazingira ya Vijijini yanaendelea kutolewa ili kupata ujuzi na matumizi ya teknolojia ya kisasa kwani vifo vitokanavyo na uzazi havikubaliki.
Mradi huo unatekelezwa katika mikoa ya Manyara, Shinyanga,Tabora, Geita, na Mwanza.



