JWTZ, polisi waanza doria Ziwa Tanganyika

KIGOMA: Utekelezaji wa mpango wa doria ya pamoja baina ya Jeshi la Polisi na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ)  umeanza katika Mwambao wa ziwa Tanganyika ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Mkuu wa mkoa Kigoma kukabili vitendo vya uhalifu na uporaji wa zana za uvuvi vinavyofanywa kwenye mwambao wa Ziwa Tanganyika mkoani Kigoma.

Uzinduzi wa mpango huo umefanyika kwenye Mwalo wa Muyobozi kijiji cha Mwakizega Wilaya ya Uvinza mkoani Kigoma ukiongozwa na Mkuu wa Wilaya hiyo, Dinnah Mathamani ambaye alisema kuwa vilio na malalamiko ya wananchi kuhusu wizi na uporaji wa zana za uvuvi umefika mwisho.

Alisema pamoja na kufanyika kwa doria hiyo pia vyombo vingine vya ulinzi na usalama ikiwemo Idara ya Uhamiaji vitaendelea na majukumu yake ikiwemo kukagua watu wote wanaoishi na kufanya kazi kwenye vijiji vya mwambao wa Ziwa Tanganyika na watakaobainika kuishi bila kufuata taratibu watachukuliwa hatua za kisheria.

Alisema kutakuwa na watendaji wa kikosi cha Zimamoto na Uokoaji ambao watatoa elimu ya ukoaji ndani ya maji, matumizi ya maboya ya kujiokolea na namna ya kukabili majanga ya moto kwenye vyombo vya uvuvi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya Uvinza, Fred Millanzi alisema kuwa Halmashauri hiyo inazo boti tano ambazo zitatolewa kusaidia kwenye jukumu hilo zikigawanywa kulingana na maeneo ya kiutendaji yatakayoelezwa.

Baadhi ya wananchi waliohudhuria uzinduzi huo akiwemo Hanzuruni Baitu mvuvi katika mwalo wa Muyobozi kijiji cha Mwakizega ameishukuru serikali hususan Mkuu wa Mkoa Kigoma, Balozi Simon Sirro kwa hatua za kurudisha doria ya pamoja.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button