Meya mpya Dodoma aahidi ushirikiano
MSTAHIKI Meya wa Jiji la Dodoma, Alimwoni Chaula amelishukuru Baraza la Madiwani kwa kumpa dhamana ya kuongoza jiji hilo kwa kipindi cha miaka mitano, huku akiahidi kufanya kazi kwa ushirikiano ili kuharakisha maendeleo kwa wananchi.
Akizungumza mara baada ya kutangazwa mshindi, amesema ushindi huo ni kielelezo cha imani na atalitumikia baraza kwa uadilifu.

“Ninawashukuru sana waheshimiwa madiwani kwa kunichagua kuwa Mstahiki Meya wa Jiji letu hili la Dodoma. Haikuwa rahisi kwakweli lakini namshukuru Mungu tupo hapa. Ninaomba ushirikiano wenu ili tuweze kuongeza kasi ya maendeleo, sote tukishirikiana kazi itakuwa nzuri sana na tutaona matokeo chanya kwa haraka na kuboresha maisha ya wananchi” amesema Chaula.
SOMA: Ulega ataka kasi ujenzi miundombinu Dodoma
Meya Chaula amesisitiza kuwa anajipanga kusimamia utekelezaji wa miradi ya kimkakati, kuboresha huduma za jamii pamoja na kuimarisha uwazi na uwajibikaji ndani ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Nae, Naibu Meya wa Jiji la Dodoma, Bakari Fundikira amepongeza uundwaji wa baraza la madiwani na kuonesha imani ya ujio wa baraza jipya.
“Huu ni wakati wa kufanya kazi sasa baada ya baraza kuundwa. Tunamtegemea Mstahiki Meya wetu kuunganisha nguvu za madiwani wote bila kujali tofauti zetu na kuhakikisha tunasimamia vizuri upatikanaji wa maendeleo kwa wananchi. Tunamhakikishia ushirikiano ili wananchi wetu waone mabadiliko” amesema.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Mpunguzi, Isaya Chilongani ameahidi kumpa ushirikiano Mstahiki Meya ili kutimiza malengo ya pamoja.
“Tunampongeza Mstahiki Meya Chaula kwa kuchaguliwa. Tunaamini ataendeleza kazi nzuri ya kuleta maendeleo ya jiji letu. Tunasema kuwa Dodoma fahari ya watanzania ambapo kuna uwekezaji wa kasi sana, maboresho ya miundombinu na shughuli nyingi za kukuza uchumi zinafanyika kwa maana hiyo baraza tupo tayari kushirikiana naye bila shaka,”



