Mitandao ya kijamii kutumika elimu kuhusu Muungano

DODOMA; SERIKALI imepanga kuongeza nguvu katika kutoa elimu ipasavyo kuhusu masuala ya Muungano kwa kutumia njia mbalimbali ikiwemo mitandao ya kijamii.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Khamis Hamza Khamis, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Mwera, Zaharo Mahemed Haji, aliyehoji ni lini serikali itautaarifu umma kuhusu changamoto za Muungano zilizopatiwa ufumbuzi, ili wanasiasa wasitoposhe umma .

“Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais imeendelea na program za kutoa elimu kwa umma kupitia hotuba za viongozi wakuu, makongamano, maonesho maalum, utayarishaji wa vipindi vya televisheni, redio magazeti, uandishi na uchapishaji wa vitabu ikiwemo kitabu cha hoja zote zilizopatiwa ufumbuzi kwa lengo la kutoa taarifa kuhusu changamoto zilizopatiwa usumbufu.

Advertisement

“Aidha, katika bajeti ya mwaka 2024/25 ofisi imepanga kuongeza nguvu katika kutoa elimu kwa kutumia ipasavyo mitandao ya kijamii, vikao na makundi maalum, ziara za kimafunzo na makongamano.

“Hoja zilizopatiwa ufumbuzi zimewekwa kwenye tovuti ya Ofisi ya Makamu wa Rais, ambayo ni (www.vpo.go.tz),” amesema Naibu Waziri.