Katika Kusherehekea Sikukuu ya kuzaliwa kwake Yesu Kristo ,(Krismas) Kanisa Katoliki Parokia ya Moyo Safi wa Bikira Maria lililopo Unga ltd katika Jimbo Kuu la Arusha safi limefungisha ndoa 15 kwa mkupuo ,huku Paroko wa Kanisa hilo,Padri Festus Mangwangwi akiwapa miezi mitatu wanandoa hao, kuhakikisha ndoa zao zinajibu kwa kupata ujauzito.
Aidha kanisa hilo pia limebatiza watoto wachanga wapatao 70 ikiwa ni ishara ya kuendelea kukua na kukubalika kwa kanisa hilo duniani.
Katika Mahubili yake Padri Mangwangi alisisitiza kwa kila muumini kutoishi maisha ya kipagani bali waishi maisha ya ndoa yenye kumpendeza Mwenyezi Mungu na kwamba aliyewaunganisha Mwenyezi Mungu binadamu asiwatenganishe
𝙿𝚊𝚍𝚛𝚒 huyo,alitoa miezi mitatu kwa kila bi harusi aliyefunga ndoa leo kanisani hapo kuhakikisha ananasa Ujauzito na baada ya muda huo anataka kushuhudia agano hilo kanisani.
Kwa kuonesha hatanii aliwataka wanandoa wa kike kushika kipaza saiti na kumhakikishia mume wake kwamba atamzalia watoto bila kikoma hadi mayai ya uzazi yatakapoisha.
“Mume wangu … nipo tayari kukuzalia hadi mayai ya uzazi yaishe”ni moja ya agano la wanandoa hao wakitamka kanisani.
Alisisitiza kwa wanandoa hao kuishi maisha mema ya kumcha mungu na kuwa na hofu ya mungu, kuwa watii kwa kila mwenza na kushirikiana kwa kila jambo.
Alisema siri ya kanisa hilo kufungisha idadi kubwa ya ndoa mara kwa mara ikitanguliwa na ndoa 53 zilizofungwa agosti mwaka huu,alisema ni kutokana na ukaribu wa mapadri na waumini wake na kutaka kujua changamoto za waumini wao,uwazi wa mapato ya kanisa pamoja na kutekeleza kwa vitendo maelekezo ya viongozi wao.
Naye Padri Wakili,Damian Ndege alisema sherehe za kuzaliwa Yesu Kristu zimeenda sanjari na kubatiza watoto wapatao 72 ikiwa ni sehemu ya kukua kwa imani ya Kanisa Katoliki.
Aliwasisitiza wazazi kuwalea watoto hao katika misingi ya imani ya Kikristu ili kuwaepusha na matendo maovu yasiyompendeza Mungu.