Prof. Kamuhabwa: Mradi wa HEET umeleta mageuzi MUHAS

DAR ES SALAAM: Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) kimepiga hatua kubwa katika kuboresha elimu ya afya nchini kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET), unaotekeleza ujenzi wa Ndaki ya Tiba katika Kampasi za Mloganzila na Kigoma.

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi huo, Makamu Mkuu wa Chuo, Profesa Appolinary Kamuhabwa, alisema mradi huo umeleta mapinduzi makubwa katika mitaala na miundombinu, hatua inayotarajiwa kuongeza idadi ya wataalamu wa afya na kupunguza gharama za matibabu nje ya nchi.

“Kupitia HEET, tumeboresha mitaala 83 na kuanzisha mipya 23, pamoja na kuwapeleka wahadhiri 33 kwenye mafunzo ya juu ndani na nje ya nchi ili kuongeza uwezo wa kufanya tafiti za kisayansi,” alisema Profesa Kamuhabwa.

Alibainisha kuwa kukamilika kwa ujenzi wa Ndaki ya Tiba kutaiwezesha MUHAS kuongeza wanafunzi wa fani za afya kutoka 350 hadi 1,000 kwa mwaka, sambamba na kuimarisha huduma za utalii tiba kupitia vituo vya moyo, figo na saratani.

Kwa upande wake, Mratibu wa Mradi wa HEET wa MUHAS, Profesa Erasto Mbugi, alisema kuwa kukamilika kwa majengo na vifaa katika kampasi hizo kutarahisisha upatikanaji wa mazingira bora ya kujifunzia na kufanya tafiti, hali itakayopunguza gharama na muda wa mafunzo kwa wanafunzi.

“Wanafunzi watakuwa na fursa ya kujifunza kwa vitendo katika mazingira yanayofanana na hospitali halisi, jambo litakalowaandaa vyema kwa kazi za kitaalamu,” alisema Profesa Mbugi.

Katika Kampasi ya Kigoma, ujenzi unahusisha jengo la utawala na taaluma lenye ofisi 120, ukumbi wa mihadhara wa watumiaji 300, maktaba na TEHAMA kwa watumiaji 60, maabara sita za kufundishia, jengo la anatomia la watumiaji 300, pamoja na bweni la wanafunzi 110 na bwalo la chakula la watumiaji 150. Pia, ujenzi wa miundombinu ya barabara na uwanja wa mpira wa miguu umefanyika ili kukamilisha mazingira ya kujifunzia.

Wananchi wa maeneo jirani na miradi hiyo wameshukuru serikali na MUHAS kwa kuleta maendeleo makubwa, wakisema mradi huo umefungua fursa nyingi za ajira na kuongeza kipato cha jamii.

“Tumeona vijana wengi wa hapa wakipata ajira za muda na kudumu kutokana na ujenzi huu. Huu ni mradi wa neema kwa wananchi,” alisema mmoja wa wakazi wa Mloganzila.

Mradi wa HEET unaendelea kuwa mfano wa mafanikio katika kuunganisha elimu, utafiti na maendeleo ya kiuchumi, ambapo Serikali inalenga kutumia elimu ya juu kama kichocheo cha uchumi wa viwanda na afya bora kwa wote.

“Tunaamini kuwa kupitia uwekezaji huu, Tanzania itapunguza rufaa za wagonjwa nje ya nchi, kukuza utalii tiba na kuongeza mapato ya Taifa,” alihitimisha Profesa Kamuhabwa.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button