Rais Samia atoa Sh Mil 10 washindi mashindano ya Quran

DAR ES SALAAM; Rais Samia Suluhu Hassan ametoa zawadi ya Sh milioni 10 kwa washindi wa kitaifa wa mashindano ya kuhifadhi Quran, akiongezea katika zawadi zilizotolewa na wadau wengine ikiwemo nyumba kwa washindi wa kwanza juzuu 30.

Hayo yamesemwa leo na Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu, ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye mashindano hayo ukumbi wa Diamond Jubilee Dar es Salaam, ambapo washiriki walishindana kuhifadhi Qurani  katika makundi ya kuanzia juzuu tatu, tano, kumi, 20 na juzuu 30.

Amesema kiasi hicho cha fedha watagawana mshindi wa kwanza juzuu 30 kwa wanaume, Amiri Maulid Dundo wa Dar es Salaam na mshindi wa kwanza juzuu 30 kwa wanawake, Saima Hassan Suleiman pia wa Dar es Salaam.

Waziri Ummy ameipongeza taasisi ya Aisha Sururu Foundation (ASF) kwa kuandaa mashindano hayo na kusisitiza umuhimu wa amani na utulivu katika jamii, pamoja na kueleza umuhimu wa kumcha Mungu.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Amana Bank, Aboubakar Athuman Ally, amesisitiza umuhimu wa muongozo wa Quran katika masuala ya kiuchumi na fedha, akielezea mifumo ya kanuni za kimaadili za benki za Kiislam ambayo Amana Bank inatoa huduma zake kwa kuzingatia miongozo hiyo yenye katuoa huduma kwa haki bila kushirikisha riba.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania, Sheikh Alhad Mussa Salum amesisitiza umuhimu wa kuishi kulingana na mafundisho ya Quran katika kujenga maadili bora, hasa kwa vijana kwani ndio chanzo cha kuwa na Taifa lenye maadili mema yatayoleta amani na mshikamano.

Habari Zifananazo

Back to top button