TAASISI ya Ithibati ya Jumuiya ya nchi za Kusini mwa Afrika (SADCAS) imethibitisha na kuzipatia vyeti vya umahiri maabara nane za Shirika la Viwango Tanzania (TBS).
Akizungumza na HabariLeo leo Januari 25, 2024 jijini Dar es Salaam, Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Ithibati ya Jumuiya ya Nchi za Kusini mwa Afrika ( SADCAS) Eva Christine Gadzikwa amesema vyeti hivyo vya umahiri vilivyotolewa na hatua nzuri kwa Tanzania ambayo inathihirisha kuwa maabara hizo zinaendelea kukubalika popote duniani jambo linaongeza chachu katika uwezeshaji biashara ndani na nje ya nchi.
Amesema, maabara hizo nane zitaendelea kusaidia na kurahisisha biashara kwani majibu ya maabara hizo yataweza kukubalika na kutumika popote duniani.
“Hakuna haja tena ya kupima bidhaa zilizoidhinishwa hapa Tanzania zitakaposafirishwa nje ya nchi ambapo itasaidia kwa kiasi kikubwa kuokoa muda na kulinda wateja,”amesema Christine
Ne, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS) David Ndibalema amesema kuwa wanafuraha kubwa ya kupokea vyeti vya umahiri ambavyo vitasaidia kutambulika kimataifa kwa huduma zinazotolewa na shirika hilo, itasaidia bidhaa zinazozalishwa nchini kuingia katika ushindani kwenye masoko ya nje na ndani ya nchi.
“Kama wote tunavyotambua Tanzania ni wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na mahusiano yetu yamejikita katika biashara, lakini pia sisi ni wanachama kwenye Jumuiya ya Kusini mwa Afrika, lakini pia mwanachama wa Afrika, ambapo kwenye ngazi ya Afrika tuna soko huru la Biashara.
“Kutambulika au kupata vyeti vya umahiri ni hatua mojawapo ya kurahisisha bidhaa zetu kushindana katika masoko hayo,”amesema Ndibalema
Naye Mkurugenzi wa Upimaji na Ugezi wa (TBS) Ridhiwani Matange amesema kupata vyeti vya umahiri ni jambo kubwa la kujivunia kwani mchakato wa kupata vyeti hivyo inahitaji uwekezaji wa rasimali watu na vifaa vya kisasa na TBS imewekeza kwenye mahitaji hayo.