Samia aahidi uwanja wa ndege wa kisasa Kagera

KAGERA: MGOMBEA wa urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Dk Samia Suluhu Hassan, amesema endapo atapewa ridhaa ya kuongoza kwa kipindi kingine cha miaka mitano, serikali itaweka mkazo kwenye uboreshaji wa miundombinu kwa kuanza ujenzi wa uwanja wa ndege wa kisasa katika eneo la Kyabajwa, wilayani Misenyi, mkoani Kagera.

Akizungumza mbele ya wakazi wa Kyaka katika mkutano wa kampeni, Dk Samia alieleza kuwa uwanja huo mpya utakuwa na uwezo wa kuhudumia ndege kubwa zikiwemo aina ya Boeing 737-900, zenye uwezo wa kubeba abiria kati ya 180 hadi 220 kutoka ndani na nje ya nchi.

“Tumeanza kufanya upembuzi yakinifu kwa ajili ya kujenga uwanja mkubwa na wa kisasa katika eneo la Kyabajwa. Awali ilipendekezwa kujengwa Omukajunguti, lakini eneo hilo halikufaulu vizuri katika tathmini ya kitaalamu, hivyo Kyabajwa ndiyo limechaguliwa,” amesema Dk Samia.

Kwa mujibu wa Dk Samia, mradi huo ni sehemu ya mkakati wa kuimarisha miundombinu ya usafiri na kuchochea ukuaji wa sekta ya kilimo biashara kwa kurahisisha usafirishaji wa mazao na bidhaa kwenda masoko ya ndani na nje ya nchi.

Vilevile, alibainisha kuwa uwanja huo unatarajiwa kuchochea shughuli za kiuchumi mkoani Kagera, ikiwa ni pamoja na kuvutia uwekezaji mpya, kukuza utalii, na kuboresha huduma za usafiri wa anga kwa mikoa ya Kanda ya Ziwa na maeneo ya mpakani mwa Tanzania na Uganda.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button