Serikali: Wastaafu msilipe chochote kupata mafao

WIZARA ya Fedha na Mipango imeagiza wastaafu wasilipie chochote katika mchakato wa ulipwaji wa mafao kwa sababu huo si utaratibu wa serikali. Aidha, wizara hiyo imesema itafuatilia kwa karibu watu wanaowatapeli wastaafu hao kwa kujifanya watumishi wa wizara hiyo.
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini katika Wizara ya Fedha na Mipango, Ben Mwaipaja alisema hayo jijini Arusha jana wakati wa semina ya wahariri wa vyombo vya habari na wizara hiyo inayofanyika katika Ukumbi wa Hazina Ndogo. “Hakuna malipo yoyote yale, ni bure.
Wastaafu wasilipishwe chochote. Kuna matapeli wanaowapigia simu na kuwatapeli kuhusu malipo yao,” alisema Mwaipaja na kuongeza: “Kuna watu wanawapa taarifa na tena taarifa za uhakika kwa karibu asilimia mia moja…tunatafuta mzizi uko wapi. Hatusemi mifumo yetu haiko salama.
Lakini kuna genge la wahuni, tunalifanyia kazi.” Awali akitoa mada, Mhasibu Mkuu katika Idara ya Mhasibu Mkuu, Eugenia Jairo alisema kuna taasisi nne zinazohusika na uliipaji wa mafao. Alizitaja kuwa ni Wizara ya Fedha na Mipango (Mfuko wa Hazina), Ofisi ya Msajili wa Hazina, Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF).
Jairo alisema kwa upande wa Mfuko wa Hazina, kuna mafao manane inayoshughulikia nayo ambayo ni pamoja na kiinua mgongo, pensheni ya kila mwezi, mafao ya kifo na pensheni ya kifo. Mengine ni mafao ya wategemezi, mafao ya ajali kazini, pensheni ya ulemavu na mafao ya mkataba.
Aidha, alisema kwa upande wa Ofisi ya Msajili wa Hazina yapo mafao ya kiinua mgongo, nauli na mizigo, malipo ya mshahara na pensheni ya mwezi. Jairo alisema PSSSF ina mafao ya kustaafu, mafao ya kifo, pensheni ya warithi, mafao ya ulemavu na pensheni ya kila mwezi.
Alisema zimekuwapo changamoto ambazo zinasababisha wastaafu kuitupia lawama Hazina kwamba inachelewesha malipo yao bila kuwa na elimu. “Kuna tatizo la elimu, wastaafu wanashughulikiwa na mifuko lakini wanasema Hazina. Ni jambo ambalo wastaafu wanapaswa kulifahamu,” alisema Jairo.