Sirro ahimiza ufundishaji kompyuta vyuo vya kati

MKUU wa Mkoa wa Kigoma, Balozi Simon Sirro amevitaka vyuo vya kati vya elimu mkoani Kigoma kusisitiza ufundishaji elimu ya kompyuta, kuwezesha wahitimu wa vyuo hivyo kuwa na uelewa wa juu wa matumizi ya vifaa hivyo ili kuwasaidia katika shughuli zao baada ya kumaliza masomo.
Balozi Sirro alitoa rai hiyo akikabidhi sehemu ya kompyuta 50 kwa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo Ufundi Stadi (VETA) Kigoma, ikiwa ni utekelezaji wa ahadi yake kwa chuo hicho alipofanya ziara chuoni hapo na kukuta uwepo wa changamoto wa vifaa hivyo katika kujifunza na kufundishia.
Alisema ulimwengu wa sasa umehamia katika matumizi makubwa ya kompyuta, kurahisisha utendaji kazi na kwamba wanafunzi wa vyuo vya kati wakianza kuwa na uelewa mkubwa wa vifaa hivyo, utawapa nafasi kubwa ya kujua mambo mengi kwenye ulimwengu wa kompyuta, hivyo kuwa msaada kwa shughuli zao.

Aliwataka vijana hao kutokubali kuwa watumwa wa kutumia mafunzo ya kompyuta wanayopata kufanya mambo ya hovyo ambayo hayana tija kwa nchi na kwamba kwa kufanya hivyo, elimu watakayopata haitakuwa na tija kwa maisha yao na jamii inayowazunguka.
Akizungumza baada ya kupokea msaada huo, Mkuu wa chuo cha VETA Kigoma, Paul Kimenyi alisema kutolewa kwa vifaa hivyo kutachochea na kurahisisha ufundishaji.
Kimenyi alithibitisha kuwepo kwa upungufu wa vitendeakazi, ikilinganishwa na idadi ya wanafunzi na masomo yanayofundishwa kwa sasa ambayo sehemu kubwa yanategemea uwepo wa idadi kubwa ya kompyuta.
Kwa upande wake, Rais wa Serikali ya Wanafunzi wa Chuo cha VETA Kigoma, Amani Chaulaya alisema kutolewa kwa vifaa hivyo kutawaongezea mazingira mazuri ya kujifunza kwa kutumia teknolojia ya kompyuta, kwani masomo mengi sasa hivi chuoni hapo yanategemea uwepo wa vifaa hivyo.



