DAR ES SALAAM; TAMASHA la siku tatu kwa ajili ya kuonesha maisha ya Kiimani na mafundisho ya Krishna, ambayo yamewaleta pamoja jamii ya Kihindu kutoka kote Tanzania kwa kupitia tukio la kipekee la kitamaduni linatarajia kuanza kesho Julai 5 hadi 7 katika ukumbi wa Super Dome Masaki, Dar es Salaam.
Mwaandaji wa sherehe hizo, Yogesh Manek amesema lengo lao katika kufanikisha tamasha hilo ni kuhamasisha marafiki zao, familia, na majirani kuzingatia mafundisho ya Krishna na kuelewa kanuni za ulimwengu na Kihindu.
“Kuhamasisha vijana kushiriki katika utamaduni na kuwapa uelewa wa kina wa maadili na mafundisho ya Kihindu kupitia maisha ya Krishna duniani na kushiriki hadithi nzuri na Watanzania, na marafiki wa Tanzania.
“Tunajivunia kufanikisha tamasha linalosimulia hadithi takatifu kupitia aina za ngoma za kitamaduni kutoka India kwa hadhira ya Tanzania, kukuza uelewa wa kitamaduni na kuthamini umoja kati ya nchi hizi mbili.” amesema Yogesh Manek
Amesema katika tamasha hilo mgeni rasmi atakuwa Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi CCM Abdulrahman Kinana.
Amesema Shree Krishna Vaibhavam II, ni hadithi inayosimulia utamaduni na mienendo wa Wahindu na kuwasaidia watu mbalimbali ikiwemo Watanzania ambao ni marafiki wa karibu kujua mila na tamadunia zao.
“Kwa kipindi cha miezi 20 iliyopita, timu ya washiriki 150, ikiongozwa na Priti Punatar na Sonal Ganatra, walifanya kazi kwa bidii ili kufanya tamasha hilo liwe gumzo kutokana na kufana katika mara mbili zilizopita.
“Kile kinachofanya tamasha hili kuwa maalum ni kazi ya upendo, ushirikiano wa vipaji vya kucheza ngoma na muundo wake wa utengenezaji kwa kushirikiana na timu mbalimbali zilizofanikisha hadithi hii kutoka India .
“Shree Goverdhannathji Haveli, Tanzania Ilijengwa mwaka 2017, Shree Goverdhannathji na imekuwa kituo kikuu cha utamaduni na shughuli za kidini kwa wafuasi wa Pushtimarg kwa waumini wote wa Afrika Mashariki,” amesema.