TBA yawaita wawekezaji katika miradi yake

DAR ES SALAAM: WAKALA wa Majengo Tanzania (TBA) imetoa wito kwa wawekezaji wa sekta binafsi na Taasisi za Fedha kuwekeza katika miradi ya TBA.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es salaam wakati wa ziara ya kukagua miradi mbalimbali inayotekelezwa na TBA Mkurugenzi wa Miliki  TBA, Saidi Mndeme amesema Miradi hiyo imegharimu Sh bilioni 69.2 ambayo ni  Temeke Kota, Magomeni Kota na Masaki ambayo ilianza Septemba 2021 hadi Septemba 2023 isivyo bahati miradi hiyo haikuweza kukamilika kwa wakati kwakuwa wakala hutegemea ruzuku kutoka serikalini.

“Kwa sasa wakala upo tayari kushirikiana na sekta hizo na kabla ya mwisho wa mwezi huu tutangaza makazi ya nyumba hizi na nyumba zitakazojengwa na sekta binafsi zitatumiwa na wananchi wote.

Majengo haya yalikuwa yanatumia fedha za ndani na sasa serikali imeridhia kushirikisha sekta za fedha na sekta binafsi” amesema Mndeme

Fedha hizo zimeelekezwa kwenye miradi ya uendelezaji wa miliki kwa maana ya ujenzi wa majengo mapya ya serikali na ukarabati wa majengo ya serikali kwa ajili ya utatuzi wa makazi ya wananchi.

Vilevile Mndeme ameishukuru Wizara ya ujenzi na uchukuzi kwa usimamizi wake madhubuti kwa miradi inayoitekeleza kwa weledi wa hali ya juu.

Kuhusu mradi wa Magomeni Kota, Kaimu Meneja wa TBA Mkoa wa Dar es Salaam, Benard Mayemba amesema miradi hiyo inaendele vizuri na wameshapata fedha kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa Magomeni kota ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa majengo matano ya ghorofa.

Kwa upande wa Masaki jumla ya familia 472 zinatarajiwa kuishi katika nyumba za kisasa kuanzia chumba kimoja, viwili,vitatu na kimoja kwa ghorofa za juu zaidi.

Miradi hiyo ipo tofauti kidogo, mradi wa Magomeni ni kwa ajili ya watumishi wenye kipato cha kati na kuendelea,Temeke na Masaki ni kwa ajili ya wananchi wote wenye uwezo wakupangisha.

Mkurugenzi wa Idara ya miliki TBA, Saidi Mndeme ameishukuru serikali kwa jitihada walizozifanya kwa kuhakikisha wanaendelea kutatua changamoto ya makazi.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button