TIC yasajili miradi 16 ya bilioni 1/- Shinyanga

MWENYEKITI wa Bodi ya Kituo cha  Uwekezaji  Tanzania  (TIC ) Binilith Mahenge ameeleza Mkoa wa Shinyanga umekuwa ukifanya vizuri katika suala la uwekezaji ikiwa tayari mwaka 2024 imeweza kusajili miradi 16 yenye thamani ya Sh bilioni 1.1.

Mahenge amesema hayo leo alipotembelea kiwanda cha  kuchakata zao la pamba na kukamua mafuta cha Jielong Holdings (T) limited kilichopo eneo la N’heleghani Kata ya Kizumbi Manispaa ya Shinyanga.

Mahenge amesema kuwa Shinyanga  ipo kwenye nafasi 10 katika uwekezaji  kwa 2024  na  utaratibu ulivyowekwa na Rais baada ya  maboresho  kufanyika karibu taasisi zote  zimewekwa pamoja  ili kuwarahisishia wawekezaji.

“Nimesikia  hapa Shinyanga kuna maeneo yaliyotengwa kwaajili ya uwekezaji tutahakikisha tunahamasisha ili waje wawekeze na kiwanda hiki tumeona changamoto ni malighafi tutawashauri wakulima  waongeze bidii ya kilimo cha pamba ili kiwanda kisisimame kwaajili ya kukosa malighafi”amesema  Mahenge.

Mkuu wa mkoa wa Shinyanga  Annamringi Macha wakati ameelezea hali halisi ya uwekezaji mkoani humo alisema waliowekeza kwenye viwanda wako wengi  ila baadhi wamekuwa wakichukua maeneo bila kuyaendeleleza kwa muda mrefu na wakati mwingine kuyafugia mifugo.

Ofisa biashara Mkoa wa Shinyanga  Rose Tungu amesema  maeneo yapo mengi ya uwekezaji  yanasifa  zote na miundombinu  yote ipo  hivyo wanakaribishwa kwenye uwekezaji na hiki kiwanda kukosa malighafi wanawashauri wakulima walime sana zao la pamba soko lipo.

Kwa niaba ya Msemaji wa Kiwanda cha Jielong  Khadija Yusuph ameeleza kilianzishwa mwaka 2012  tangu kipindi hicho wamewekeza Dola za milioni 32  na kuajiri watu 30 na vibarua zaidi ya 200.

“Kiwanda kimekuwa kikisimama mara kwa mara kwa kukosa malighafi ambapo kwa sasa kinauwezo wa kutumia tani 150,000 za mbegu za pamba na upande wa jineri zimefungwa mashine 24 zinazokamua mbegu kwaajili ya mafuta”alisema  Yusuph.

Mfanyakazi wa kiwanda hicho  Hassan Manubi ambaye ni opareta amesema  amenufaika kupata ajira na kuendesha maisha kwenye familia zao kwani changamoto kuendesha kiwanda na muda mwingine kukaa nyumbani miezi mitatu hadi mitano kwa kukosa malighafi.

Habari Zifananazo

Back to top button