MAREKANI : RAIS mteule wa Marekani Donald Trump amesema atakutana na Rais wa Urusi Vladimir Putin haraka iwezekanavyo baada ya kuingia madarakani wiki ijayo.
Hata hivyo, hakutoa muda mahsusi wa mkutano huo, ambao utakuwa wa kwanza kati ya viongozi wa nchi hizo mbili tangu Urusi ilipoivamia Ukraine mnamo Februari, mwaka 2022.
Alipoulizwa kuhusu mkakati wake wa kuvimaliza vita hivyo,Trump ameuambia mtandao wa Habari wa Newsmax kuwa kuna mkakati mmoja tu na hilo litaegemea kwa Putin.
Mike Waltz, ambaye ni mshauri mpya wa usalama wa taifa alieleza siku ya Jumapili kwamba anatarajia viongozi hao wawili Putin na Trump kuzungumza kwa njia ya simu katika wiki chache zijazo. SOMA:Nitamaliza vita vya Urusi na Ukraine – Trump
Uvamizi wa Urusi nchini Ukraine umesababisha vifo vya maelfu ya watu na kuwaacha mamilioni ya wengine bila maakazi rasmi na umesababisha pia mahusiano kuvunjika kati ya Moscow na mataifa ya Magharibi tangu mgogoro wa makombora wa Cuba wa mwaka 1962.