SERIKALI imesema katika mwaka 2023/2024,itakamilisha ujenzi wa mialo minne.
Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega bungeni jijini Dodoma wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha wa 2023/2024.
Waziri Ulega aliitaja mialo hiyo na wilaya zake katika mabano kuwa ni Igabiro (Bukoba), Chifunfu (Sengerema), Igombe (Ilemela) na Kayenze (Ilemela), pamoja na vituo vitatu (3) vya Usimamizi wa Rasilimali za Uvuvi vya Sota (Rorya), Simiyu (Busega) na Nyakaliro (Sengerema).
“Aidha, serikali itafanya upembuzi yakinifu wa ujenzi wa soko la samaki Kigamboni na maeneo nane ya ujenzi wa miundombinu ya Ofisi za Ulinzi wa Rasilimali za Uvuvi Kigoma, Tanga, Mtwara, Muleba, Kagera, Mtera, Ikola, na Singida,” amesema Waziri Ulega.