Wadau wajadili mabadiliko tabianchi kwenye kilimo nchini

JUKWAA la Wakurugenzi wakuu wa Kampuni Tanzania (CEOrt) kwa kushirikiana na Umoja wa Kimataifa wa Uhifadhi wa Mazingira (IUCN) na Mpango wa Ukuaji wa Kilimo katika Ukanda wa Tanzania (AGCOT) limeandaa warsha ya ngazi ya juu jijini Dodoma kujadili changamoto za mabadiliko ya tabianchi kwenye kilimo.
Warsha hiyo imehusisha viongozi kutoka sekta za kilimo-biashara, fedha na sera ili kuharakisha ujumuishaji wa suluhisho zinazotegemea asili katika maendeleo na mazingira ya uwekezaji nchini.
Akizungumzia hilo, Mkurugenzi Msaidizi wa Mazingira kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Thomas Chali amesema namna ambavyo NbS zinaweza kusaidia biashara kukabiliana na hatari za mabadiliko ya tabianchi huku zikifungua fursa mpya za ukuaji endelevu.
Washiriki walijadili mbinu za kiikolojia kama vile ‘kilimo mesto’ (agroforestry), urejeshaji wa udongo na maji, pamoja na mifumo ya uchumi zinazoweza kuimarisha mnyororo wa thamani, kupunguza hatari za kiutendaji na kufanikisha viwango vya kimataifa vya uendelevu na vigezo vya ESG (Mazingira, Jamii na Utawala Bora).
Alisema dhamira ya serikali ya kuongeza utekelezaji wa NbS ni kuwa chombo muhimu cha kufanikisha malengo ya tabianchi ya Tanzania.
“Tunapoendelea kuelekea katika malengo yetu ya kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa, suluhisho zinazotegemea asili ni njia ya vitendo na inayowezekana kuunganisha ulinzi wa mazingira na ukuaji wa kijamii na kiuchumi,” amesema.
Kupitia nguzo yake ya biashara na uendelevu, CEOrt inaweka sekta binafsi kuwa chachu ya mabadiliko ya tabianchi na mageuzi ya kijani.
“Kwa mwaka 2050, Tanzania inalenga kuwa miongoni mwa nchi tatu bora Afrika kwa kuvutia uwekezaji, kwa msingi wa ukuaji wa kijani, jumuishi, na wenye ushindani,” amesema Hawa Urungu, Meneja Miradi wa CEOrt.
Akichangia kwa upande wa sekta ya kilimo, John Nakei ambaye ni Meneja wa Ushirikiano na Mnyororo wa AGCOT, alieleza utayari wa sekta hiyo kuongeza jitihada.
“Kilimo kiko katikati ya hatari na fursa za tabianchi, kwa kutumia suluhisho zinazotegemea asili, biashara za kilimo zinaweza kurejesha rutuba ya udongo, kuboresha matumizi ya maji, na kufungua uwekezaji wa kijani,” amesema.
Ameongeza: “Mbinu hii si nzuri tu kwa mazingira; ni mbinu ya kiuchumi yenye akili inayohakikisha ushindani wa muda mrefu kwa wakulima na biashara za kilimo za Tanzania”.



