MTWARA; USAID PS3+ kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), imeandaa mafunzo ya siku tano Mkoani Mtwara kuwajengea uwezo Makatibu Tawala Wasaidizi wa Mikoa, Maofisa TEHAMA na Makatibu Tawala sehemu ya usimamizi, ufuatiliaji na ukaguzi.
Mafunzo hayo yameanza leo kwa lengo la kusaidia washiriki kujifunza juu ya mifumo mbalimbali ya sekta ya umma iliyoboreshwa.
Baada ya mafunzo, washirika (RS) wataweza kwenda kuzisimamia halmashauri katika utekelezaji wa mifumo pamoja na suala zima la ushirikishwaji wa wananchi na utawala bora.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo Katibu Tawala Msaidizi mkoani, Mtwara Robert Misungwi ameishukuru USAID PS3+ kwa ufadhili wa mafunzo hayo, huku akisema yatasaidia kuongeza ufanisi kwa washirika katika majukumu yao na kufanya suala la matumizi ya mifumo kuwa endelevu.
Mafunzo hayo yamehusisha washiriki kutoka Mtwara, Lindi, Pwani, Dar es Salaam, Ruvuma, Mbeya na Njombe.