Wanafunzi kidato cha 4 wafa ajali ya bodaboda, lori

MOROGORO; WANAFUNZI wawili wa kidato cha nne wa Shule ya Morogoro Sekondari, Lusajo Mwang’onda (18) na Ghalib Omary (18) wakazi wa Kata ya Kihonda Maghorofani , Manispaa ya Morogoro wamefariki dunia kutokana na ajali ya bodaboda iliyowabeba kwenda shule kuparamia lori barabara kuu ya Morogoro- Dodoma.
Dereva wa bodaboda hiyo, Baraka Sijawaza Sajio (22) pia mkazi wa Kihonda Maghorofani, naye alifariki dunia papo hapo kwenye ajali hiyo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Alex Mkama amesema ajali hiyo imetokea leo Julai 18,2025 saa moja asubuhi eneo la Samaki Samaki Bima.

Amesema pikipiki yenye namba za usajili MC.534 DYX, ikiendeshwa na Sajio ikitokea Kihonda kwenda Morogoro mjini, ikiwa imewabeba abiria wawili iligongana na gari lenye namba za usajili T .310 DQC lenye tela T.646 ANQ likiendeshwa na Simba Omary Juma, (45) mkazi wa Tandale Dar es Salaam.
Ametaja chanzo cha ajali hiyo ni uzembe wa dereva wa bodaboda kujaribu kuyapita magari mengine bila kuchukua tahadhari.



