Waomba mazingira bora zaidi elimu jumuishi

WADAU wa Maendeleo ya Sekta ya Elimu wameiomba Serikali kujenga vituo vya ubainishaji na upimaji kwa watoto wenye ulemavu na mahitaji maalumu ngazi ya Halmashauri ili kuwafikia watoto wengi zaidi wanaotakiwa kujiunga na shule za awali na msingi.
Wametoa rai hiyo mjini Morogoro katika kikao cha tathimini na kukabidhi mradi wa elimu jumuishi (TASK ORDER 51) uliokuwa ukitekelezwa katika Manispaa ya Shinyanga, Halmashauri ya Shinyanga na Halmashauri ya Misungwi, mkoani Mwanza katika kipindi cha mwaka 2022 hadi 2025.

Elimu jumishi ni mchakato unaolenga kuongeza ushirikishwaji katika ujifunzaji kwa watoto wote wakiwemo wenye mahitaji maalumu ili waweze kujifunza bila vikwazo.
Mratibu wa mradi huo, Gerald Tuppa amesema kwa kipindi hicho, mradi huo umejenga vituo vya ubainishaji na upimaji vitatu katika halmashauri hizo.
SOMA: Mtwara watakiwa kuzingatia elimu kwa watoto
Tuppa amesema vituo hivyo vimesaidia upimaji watoto wenye uhitaji maalumu 1,864 ambapo kati yao 1,468 walinufaika na mradi huo kwa kuandikishwa shuleni kupata elimu na wengine kupatiwa vifaa saidizi.
“Vituo hivi vinapima mahitaji ya kielimu kwa sababu mtoto mwenye ulemavu kila mmoja anatofautiana, kwa hiyo kuna umuhimu kubwa kwa Serikali kuwekeza katika vituo vya upimaji ili kabla mtoto hajapelekwa darasani apimwe kujua anahitaji usaidizi wa namna gani,” anasema Tuppa.

Tuppa amesema kupitia mradi huo kumekuwa na mafanikio mengi katika halmashauri hizo kwa kuwezesha vifaa saidizi kwa wanafunzi 121 kwa kupatiwa viti mwendo, miwani, visaidizi vya kusikia na vifaa bandia.
Mratibu wa mradi huo, amesema jumla ya shule za msingi 15 zimenufaika kwa kuwekewa miundombinu wezeshi ikiwemo ujenzi wa vyoo na ukarabati wa madarasa ya kujifunzia.
Kwa upande wake Ofisa Tathimini na Ufatiliaji kutoka Shirika la Light for the World la Kenya, Wycliffe Nyakundi amesema ushiriki wao katika mradi huo umesaidia kwa kiasi kikubwa kuongeza nguvu katika kuhamasisha jamii kujitokeza kuandikisha watoto wenye mahitaji maalumu kujiunga na shule.

Nyakundi anasema njia zilizotumika kuhamasisha jamii ili kuandikisha watoto wao ni shirikishi kupitia kwa walimu na taasisi za watu wenye ulemavu na kwa kiasi kikubwa kuliwafanya wazazi kutambua umuhimu wa elimu kwa watoto wao tofauti na awali walipokuwa wakiwaficha na kuwanyima watoto haki ya kupata elimu.
“Tumefarijika kuona hata walimu tulipowashirikisha na kuwapatia mafunzo wamekuwa mstari wa mbele kuhamasisha wazazi na kuwahudumia wanafunzi wenye mahitaji maalum, hivyo tunaomba Serikali kuendelea pale mradi ulipoishia kwa sababu wazazi wengi wamehamasika kuandikisha watoto wao baada ya kuona taasisi za wenye ulemavu zinashirikishwa” amesema Nyakundi.



