Wasichana 6,685 waliokatisha masomo warejea shuleni

WASICHANA 6,685 wenye umri kati ya miaka 13 na 21 waliokatisha masomo ya sekondari kwa sababu mbalimbali ukiwemo ujauzito wamejisajili kuendelea na masomo kwa njia mbadala chini ya Mradi wa Kuimarisha Ubora wa Elimu ya Sekondari (SEQUIP- AEP).

Wasichana ahao wamesajiliwa  ndani ya kipindi cha miaka miwili  ya utekelezaji wake ulipoanza  rasmi mwaka 2022.

Mkurugenzi  Mkuu wa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW) Dk Michael Ng’umbi amesema  hayo  Machi 2, 2023 mjini Morogoro   wakati wa uzinduzi wa  Baraza la 13  Wafanyakazi wa Taasisi hiyo.

Advertisement

Dk  Ng’umbi amesema  mradi huo unaotekelezwa na Taasisi hiyo ulianza mwaka jana (2022)  na ulisajili wasichana 3,333 walianza masomo hayo na wanaendelea na masomo  katika   vituo mbalimbali vya taasisi hiyo nchini.

Mkurugenzi mkuu wa Taasisi hiyo amesema  kwa  mwaka wa  masomo wa 2023 na  hadi kufikia  Februari mwishoni wasichana 3,352  tayari wamejisajili kuendelea na masomo yao.

“ Tumepata mafanikio makubwa tangu kuanza kwa mradi kwani  katika kipindi cha mwaka jana (2022 ) kwa  kuvuka lengo  kwa kuwasajili  wasichana 3,333 ambao  wanaendelea na masomo yao ” amesema Dk Ng’umbi

Dk Ng’umbi amesema  mradi huo  unalenga kunufaisha wasichana 12, 000 nchini ambapo kila mwaka utasajili wanafunzi 3,000 kwa kipindi cha miaka mitano  kuanzia 2022 hadi kufikia mwaka 2026 .

Mradi huo  unalenga kuwapatia elimu ya sekondari bila malipo wasichana waliokatisha masomo ya elimu ya sekondari kwa sababu mbali mbali ikiwemo  kupata ujauzito au hali ngumu ya maisha.

Dk Ng’umbi ameiomba  serikali kuangalia uwezekano wa kugharamia  ujenzi wa Hosteli , na kutoa chakula kwa wasichana hao ili kiwe kichocheo cha kuudhuria masomo hayo ili kufanikisha malengo yaliyokusudiwa.

Serikali ya awamu ya sita ya Rais Dk Samia Suluhu Hassan iliwaondolea vikwazo  wanafunzi wa shule za msingi na sekondari  waliokatisha  masomo kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo kupata ujauzito.

Mradi huo unatekelezwa na taasisi  hiyo  iliyopo  chini ya Wizara ya Elimu ,Sayansi na Teknolojia kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TEMISEMI) kwa ufadhili wa Benki Dunia.

Add a comment

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *