Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika mkoani Katavi, Onesmo Buswelu amewataka wavuvi wanaovua Samaki ziwa Tanganyika kuacha tabia ya kufanya uvuvi haramu badala yake watumie zana sahihi za uvuvi kwa ajili ya uvuvi endelevu.
Ametoa agizo hilo alipokuwa akizungumza na wananchi wa Karema wakati akizindua ofisi ya Usimamizi shirikishi wa rasilimali za uvuvi (BMU) Kata ya Karema na kuwatunuku vyeti wawakilishi wa uhitimu wa Askari 14 wa majini (Village Game Scout) kwa ajili ya kusimamia na kulinda mazalia ya samaki katika ziwa Tanganyika na kudhibiti uvuvi haramu.
“Kwa wasiopenda kufuata sheria na taratibu wabadilike, wasipodadilika tumeambiwa hapa kuna sero ya kuanzia,itatumika kwa hao, fuata taratibu,fuata sheria ili tuweze kuwa na uvuvi endelevu ili ziwa hili na rasilimali iliyoko pale iweze kutupatia manufaa”amesema
Aidha,ametoa wito kwa wananchi wa Karema kuitumia fursa ya mazao ya samaki kutoka Ziwa Tanganyika kwa kujiingizia kipato kwa kuwa soko lipo la kutosha na miundombinu ya barabara imefunguka.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa programu ya TUUNGANE Lukindo Hiza,amesema kama taasisi wamejenga ofisi hiyo ya BMU iliyoghalimu zaidi ya Tsh. Milioni 56 lengo likiwa ni kuinua usimamizi mzuri wa uhifadhi na unufaikaji endelevu wa mazao ya uvuvi ikiwa ni pamoja na kufadhili mafunzo ya walinzi 14 wa jamii ambayo yameghalimu takribani milioni 3.5 kwa kila mmoja.
Hiza amesema,mikakati yao ni kuwezesha mfumo utakaowezesha kufanya utafiti wa vyombo vya uvuvi vinavyotumika ziwani ikiwemo kutambua wavuvi wako kwenye mwalo upi ambapo mchakato huo ukikamilika unaweza kuongeza udhibiti uvuvi haramu kama siyo kutokomeza kabisa.