Miundombinu utalii kuimarishwa AFCON 2027

ARUSHA: WAKALA wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo ya utalii ikolojia wameanza kuimarisha miundombinu ya utalii na uwekezaji wa kuongeza maeneo ya malazi ili kuchangamkia fursa ya Mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) mwaka 2027.
Ofisa Utalii Hifadhi ya Misitu Ziwa Duluti kutoka TFS ,Batholomeo Msensemya, amesema hayo hifadhini hapo kuwa maboresho hayo ni mkakati wa kuhakikisha Tanzania inanufaika kikamilifu na michezo hiyo.

Tanzania inatarajiwa kuwa mwenyeji wa mechi za Afcon 2027 katika viwanja vya Dar es Salaam, Dodoma na Arusha pamoja na Nchi za Kenya na Uganda.
Msensemya amesema uboreshaji wa miundombinu hiyo inalenga kuhudumia idadi kubwa ya wageni watakaofika nchini, jambo litakalozalisha ajira kwa jamii na kuongeza mapato ya Taifa kupitia vivutio mbalimbali vikiwemo wa Hifadhi ya Misitu Ziwa Duluti mkoani Arusha.

Amesema TFS imejipanga kwa ujio huo na moja ya vitu vinavyofanyika kwa kushirikiana wadau ni uwekezaji kwenye malazi ambapo wawekezaji wanajenga hoteli na nyumba za kulala wageni “lodges” ndani ya hifadhi hiyo.
Msensemya amesema hatua hiyo itaongeza wigo watalii kulala ndani ya eneo la hifadhi za Msitu huu na mpaka sasa zimejengwa unit 30 zenye kuweza kulaza watu mpaka 60 kwa siku.

Amewashauri vijana kujiandaa kuwekeza zaidi kwenye mitumbwi au boti ili kuwezesha utalii wa kuendesha mitumbwi na michezo ya kuvua samaki katika Ziwa Duluti, vijana wa bodaboda kujipanga vyema, wauzaji vinyango na mama lishe namna ya upikaji vyakula vya asili.
“Katika hifadhi yetu pia kuna ziwa , ni fursa kwa Vijana kuwekeza kuongeza mitumbwi au boti pamoja na wengine kutoka nje ambao wanawiwa kuwekeza katika hifadhi ya misitu ya Duluti na kwenye vingine wanavyoona vinavutia wageni,”amesema Msensemya.

Amevitaja vivutio vilivyopo ndani ya Hifadhi hiyo ni kutembea kuzunguka msitu wenye urefu kilometa tano ,kuendesha mitumbwi, michezo ya kuvua samaki na kuangalia ndege wa aina tofauti na kuona mapango yenye historia .
Wakati huo huo, Meneja wa Michezo na Burdani wa Meru Eco Camp, Maxmilian Thobias amesema kuelekeza Afcon mwakani, mpango kazi wa uwekezaji makazi kwa maana ya malazi kwa kutengeneza nyumba za kulala wageni “lodges” za kisasa zinazoendana na uhifadhi wa mazingira ikolojia umeandaliwa.

Thobias amesema Meru Eco Camp imejengwa ndani ya Msitu wa Hifadhi Meru unaomilikiwa na TFS ambao una vivutio vingi vya utalii yakiwemo maporomoko ya m aji unayofahamika kwa jina la Napuru.
“Meru eco Camp tumejipanga kwa kuboresha shughuli nyingi zinazopatikana na kuongeza nyingine zikiwemo za kisasa zaidi yakiwemo malazi ( Camping) kwa wageni wengi,”amesema Thobias.
Kwa upande wake Msimamizi wa Huduma za Chakula, Emmanuel Mabula kwa niaba ya wafanyakazi ameishukuru Serikali kupitia TFS kwa hamasa ambayo imeiweka kupitia utalii ambao umeleta mchango mkubwa kwa wananchi na kutoa ajira kwa vijana.
“Tunaishukuru Serikali kuileta AFCON ijayo jijiji Arusha ,Meru Eco Cam imejindaa kutumia fursa iliyoandaliwa na Serikali kwa kuandaa Afcon ,tutaitumia vyema kuendeleza utalii hasa wa kimazingira kwa kuvutia wageni wengi kwa malazi na chakula,” amesema Mabula.


