Azungumzia nafasi ya wanahabari PPP

DAR ES SALAAM: Mwandishi mkongwe nchini, Eda Sanga, amewakumbusha wadau wa sekta ya umma na binafsi kuhusu nafasi isiyozibika ya vyombo vya habari katika kufanikisha mageuzi ya utoaji huduma za afya kupitia mfumo wa Ubia (PPP).
Sanga ametoa ushauri huo wa kimkakati wakati akichangia mada katika Kongamano la Kitaifa la PPP katika Sekta ya Afya lililofanyika katika Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS), jijini Dar es Salaam.
Akielezea utekelezaji wa Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo (FYDP IV) na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Sanga aliweka wazi kuwa dhana ya PPP ni mpya kwa walio wengi, hivyo inahitaji uelewa wa kina.
Aliwaasa wataalamu wa PPP-Centre kuwekeza katika kuwapa mafunzo waandishi wa habari ili waweze kuhabarisha jamii kwa usahihi.
Sanga alieleza kikwazo kikubwa kinachofanya wananchi wa kawaida wasielewe miradi mikubwa ya uwekezaji kuwa ni matumizi ya misamiati migumu ya kitaalamu.
Aliviomba vyombo vya habari na wataalamu kutumia lugha rahisi na rafiki pamoja na ubunifu katika kuwasilisha taarifa zinazohusu afya na uwekezaji wa sekta binafsi.



