‘Tutaendelea kujenga ofisi za kisasa, zenye hadhi’

KATIBU wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya Chama cha Mapinduzi (CCM), NIdara ya Organaizesheni, Komredi Issa Haji Ussi Gavu amesema CCM itaendelea na ujenzi wa Ofisi za Chama hicho zenye hadhi na za kisasa.
Akizungumza katika ujenzi wa Taifa Ofisi ya Tawi la CCM Cheju Chuchumile Jimbo la Chwaka Mkoa Kusini Unguja, Komredi Gavu amesema CCM ni chama kikubwa hivyo ni jambo la msingi ofisi za chama kuanzia ngazi zote kuwa zenye hadhi kubwa.
” Leo tumekuja hapa kwa ajili ya kushiriki ujenzi wa Taifa wa ofisi yetu ya tawi, nakuombeni tuendelee kujenga matawi kama haya,” alisema Komredi Gavu.
Katibu huyo wa Idara ya Oganaizesheni ambaye pia ni Mwakilishi wa Jimbo la Chwaka, amewaambia Wana CCM katika Kijiji hicho kuwa ni wajibu wa kila mwanachama kuhakikisha anashiriki katika uimarishaji wa Chama.
Komredi Gavu amewahakikishia kuwa nao bega kwa bega kuleta maendeleo katika JImbo hilo.
Aidha, Komredi Gavu amewataka wananchi wa Jimbo la Chwaka kuendelea kutembea kifua mbele huku wakielezea mafanikio ya Serikali ya Awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan.
” Wana CCM tuna kila sababu ya kutembea kifua mbele, Mwenyekiti wetu na Rais wetu Mhe Mama Dk Samia Suluhu Hassan anafanya mambo makubwa katika ujenzi wa nchi yetu, tunakwenda vizuri tuna kila sababu ya kumpongeza Rais Dk Samia,” Alisema Komredi Gavu.
Mwenyekiti wa CCM Jimbo la Chwaka, Mwalimu Mpima amesema kuwa ujenzi wa Ofisi ya Tawi la Cheju Chuchumile utagharimu zaidi ya shilingi milioni 100.
Mwenyekiti huyo amesema mbali ya nguvu za wananchi katika ujenzi wa ofisi hiyo, Mwakilishi wa Jimbo la Chwaka Komredi Gavu ametoa fedha za awali za ujenzi wa Ofisi hiyo na ameahidi kuendekea kutoa fedha nyengine kwa ajili ya kukamilisha ujenzi.



