Azania benki yatoa mikopo ya bil 3/- , Iringa – Mkuu wa Mkoa atoa wito

IRINGA: Benki ya Azania imefanikisha kutoa mikopo yenye thamani ya zaidi ya Sh bilioni 3 kwa wananchi wa Mkoa wa Iringa katika kipindi cha miezi sita pekee tangu kufunguliwa kwa tawi lake mjini Iringa.
Hatua inayotarajiwa kuongeza kasi ya maendeleo ya kiuchumi kwa wakulima, wafanyabiashara wadogo, wafugaji, wastaafu na makundi mengine ya wajasiriamali.
Akihitimisha maadhimisho ya Wiki ya Huduma kwa Wateja katika tawi hilo la benki ya Azania, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri James, aliwataka wananchi na wajasiriamali kutumia huduma za kifedha kutoka taasisi rasmi kama benki ili kuepuka unyonyaji unaofanywa na wakopeshaji haramu maarufu kama kausha damu.

“Nitoe rai kwa wananchi wa Iringa—tuwakwepe wakopeshaji wasio rasmi wanaotumia shida za watu kujinufaisha. Tukimbilie taasisi kama Azania Benki ambazo zinatoa mikopo kwa riba nafuu na kwa uwazi,” alisema Kheri James.
Kwa upande wake, Meneja wa Benki ya Azania tawi la Iringa, Gaile Lungwa, alisema tangu kufunguliwa kwa tawi hilo miezi sita iliyopita, benki imejipanga kuhakikisha huduma za kifedha zinawafikia wananchi kwa urahisi zaidi na kwa masharti rafiki.
“Tayari mikopo ya zaidi ya bilioni tatu imetolewa kwa wananchi wa Iringa, ikiwemo kwa wanawake, wakulima, wafanyakazi na wastaafu. Lengo letu ni kuhakikisha mikopo hii inachochea shughuli za uzalishaji mali na kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja,” alisema Lungwa.

Aliongeza kuwa mikopo kwa akinamama imekuwa na masharti nafuu zaidi, ikiwa na riba ya asilimia moja kwa mwezi, huku wastaafu wakipewa kipaumbele maalum ili waweze kuendelea kushiriki katika shughuli za kiuchumi baada ya kustaafu.
“Tunaamini kustaafu si mwisho wa mafanikio. Tunatoa fursa kwa wastaafu kupata mikopo kwa uaminifu mkubwa ili waendelee kuboresha maisha yao na ya jamii inayowazunguka,” alisema.
Aidha, Lungwa alibainisha kuwa benki ya Azania, inayomilikiwa na mifuko ya hifadhi ya jamii kama NSSF, PSSSF na NHIF, imekuwa mshirika muhimu wa maendeleo katika halmashauri zote kupitia utoaji wa mikopo ya asilimia 10 ya mapato ya ndani kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.
Mikopo hiyo inatarajiwa kuongeza uzalishaji katika sekta za kilimo, ufugaji na biashara ndogondogo, na hivyo kuimarisha uchumi wa kaya nyingi katika mkoa wa Iringa.
“Tunataka kuona Iringa inakuwa kitovu cha fursa za kifedha kwa wananchi wote. Benki ya Azania iko hapa kuhakikisha kila mmoja anaweza kufikia ndoto zake kwa kutumia huduma bora za kifedha,” alisema.



